Wito wa amani kufuatia kisa cha mauaji msikitini
JAMII katika Kaunti ya Lamu zimesisitiza wito wa ushirikiano kuhubiri amani na utangamano kati yao, kufuatia kisa cha mauaji msikitini wiki chache zilizopita.
Msomi wa dini ya kiislamu na imamu, Bw Mahmoud Ahmed Abdulkadir, alisema mauaji hayo yalikiuka sheria za kimataifa zinazopinga ukatili kutekelezwa ndani ya sehemu za ibada.
Mnamo Mei 13, Khalid Makka, 33, alivamiwa na kudungwa kisu wakati wa sala ya adhuhuri kwenye msikiti wa Jamia mjini Faza, Lamu Mashariki. Alifariki akikimbizwa hospitalini.
“Hatutarajii mauaji yangetekelezwa msikitini, mazingira ambayo yanachukuliwa kuwa ya amani na utu. Lazima tukomeshe uozo kwenye jamii zetu, tuhubiri amani na umoja,” akasema Bw Abdulkadir.
Mwenyekiti wa Baraza la Maimamu na Wahubiri wa Kiislamu Nchini (CIPK) tawi la Lamu Abubakar Shekuwe, alisihi idara ya usalama kufanya hima kuhakikisha wanaoshiriki uhalifu wanachukuliwa hatua kali za kisheria.
Bi Nahida Kassim, ambaye ni Rais wa Bunge la Vijana Lamu, aliomba vijana wote kuzingatia nidhamu ili wafaulu maishani.
Naye Ustadh Abdalla Mohamed alisihi jamii ya Lamu kudumisha utu na kuheshimu dini.