Tuonane kortini tena, asema Gachagua akirarua hukumu ya majaji watatu
ALIYEKUWA Naibu wa Rais, Rigathi Gachagua, amekosoa vikali hukumu ya majaji watatu wa Mahakama Kuu iliyohusu kushtakiwa na kuondolewa kwake madarakani, akisema uamuzi huo ni “kinyume cha katiba” na “umejaa utata unaoonekana wazi na Wakenya”.
Akizungumza baada ya kupitia hukumu hiyo pamoja na mawakili wake, Gachagua alisema atakata rufaa katika Mahakama ya Rufaa akipinga kile alichotaja kuwa ni uamuzi unaojikanganya wenyewe na unaodhalilisha haki za msingi za kikatiba.
Mnamo Jumatatu, majaji watatu wa Mahakama Kuu waliidhinisha kuondolewa kwake mamlakani lakini wakasema seneti ilikiuka haki zake kwa kutoahirisha kikao alipolazwa hospitalini.
“Ni vigumu kuelewa mambo ambayo jopo la majaji watatu limetaja kuwa kinyume cha Katiba, lakini bado mahakama hiyo hiyo inasema mchakato huo ni halali. Huo ni mkanganyiko unaodharau akili ya Wakenya waliokuwa wakifuatilia kesi hii,” alisema.
Gachagua alisisitiza kuwa mchakato wa kumtimua ulihusisha ukiukaji wa wazi wa haki zake za msingi, akirejelea Ibara za 25, 47 na 50 za Katiba ya Kenya zinazohusu haki ya kusikilizwa kwa haki na bila upendeleo.
Kulingana naye, mahakama ilitambua kuwa hakupewa nafasi ya kutosha kujitetea, jambo ambalo linabatilisha mchakato mzima wa kumuondoa madarakani.
Alisema kwamba, endapo haki ya kusikilizwa inakiukwa, basi matokeo yote yanayofuata yanapaswa kubatilishwa moja kwa moja.
“Kwa mujibu wa Katiba, hasa Ibara ya 47, kila mtu ana haki ya kupata mchakato wa haki. Mahakama yenyewe ilikiri kuwa haki yangu ya kusikilizwa ilikiukwa. Hapo mchakato mzima ulipaswa kufutwa. Haukuwa halali,” alisema.
Aliongeza kuwa uamuzi wa majaji hao kuendelea kuthibitisha matokeo ya mchakato huo licha ya kugundua dosari za kikatiba ni “kinyume cha wajibu wa Mahakama” chini ya Ibara ya 165 ya Katiba.
“Ni ajabu kuona mahakama ikisema haki ya kusikilizwa ilikiukwa, lakini bado ikathibitisha matokeo ya mchakato huo huo. Huo ni mkanganyiko wa kikatiba usioelezeka,” aliongeza.
Gachagua alitaja mchakato huo “mapinduzi ya kikatiba” akidai ulikuwa ni njama iliyolenga kumuondoa madarakani kwa njia zisizo halali.
Alisema mchakato mzima uliporomoka mara tu mahakama ilipokiri kuwepo kwa ukiukaji wa haki zake.
Katika mkutano wake na wanahabari na mawakili wake, Gachagua alithibitisha kuwa tayari amewapa maagizo ya kukata rufaa katika Mahakama ya Rufaa, akisisitiza kuwa vita hivi ni vya kikatiba na si vyake binafsi.
“Tumechambua hukumu hii na tumekubaliana kuwa tutaenda Mahakama ya Rufaa. Lengo letu ni kutaka haki itendeke na mchakato huu usio wa kikatiba ubatilishwe,” alisema.
Aliongeza kuwa anaendelea kupokea uungwaji mkono kutoka kwa wafuasi wake na Wakenya mbalimbali wanaohoji hali ya kisiasa iliyoibuka baada ya uamuzi huo.
Kulingana naye, kumekuwa na taarifa potofu zinazodai kuwa hawezi kugombea urais, akizitaja kama propaganda za kisiasa.
Alisisitiza kuwa chini ya Ibara ya 99 ya Katiba, hakuna mtu anayepaswa kuzuiwa kugombea uchaguzi kabla ya rufaa zote kukamilika.
Alisema yuko tayari kuwania urais katika uchaguzi ujao wa 2027 iwapo muafaka wa kisiasa ndani ya muungano wa upinzani utamteua kupeperusha bendera yao.
Gachagua pia alitoa mfano wa mtafaruku huo akilinganisha na hali ambapo mtu anashtakiwa bila haki ya kusikilizwa, akifungwa, kisha baadaye mahakama inakiri kuwa kesi hiyo haikuwa ya haki.
Alisema fidia ya Sh50 milioni aliyopewa na mahakama ni “kejeli kwa haki za kikatiba” na haiwezi kulinganishwa na madhara aliyopitia.
“Sisi hatutafuti pesa. Hii si kuhusu fidia. Ni kuhusu haki na utawala wa Katiba. Hata niliwahi kupewa Sh2 bilioni mbili ili nijiuzulu, lakini nilikataa. Haki haiuzwi,” alisema.
Alitangaza kuwa atarudi Wamunyoro “kujipanga upya kisiasa na kijamii,” huku akisisitiza kuwa eneo hilo ni ngome yake ya msingi ya kisiasa na mahali ambapo uamuzi wake wa hatua zinazofuata utajengwa.
“Naenda Wamunyoro kushauriana na wafuasi wangu kwa siku 45, kupanga mikakati ya hatua zinazofuat,” akasema.
Bw Gachagua alisema atahakikisha muungano wa upinzani umeteua mgombea urais mmoja kumenyana na Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027 akiapa kuwa asipopata tiketi, ataunga atayeteuliwa na kumpigia debe kwa hali na mali.