Habari za Kitaifa

Maswali kuhusu ujenzi wa vituo 22 vya Ebola ikihofiwa huenda ni hewa

Na ANGELA OKETCH June 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI imekuwa ikitetea ujenzi wa kituo cha kutenga wagonjwa wa Ebola katika Kambi ya Jeshi Laikipia, Nanyuki, kwa wiki kadhaa, lakini sasa imekumbwa na maswali mapya kuhusu vituo vingine 22 ambavyo ilisema vinajengwa kama sehemu ya mpango wa kitaifa wa kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa huo.

Waziri wa Afya Aden Duale, amesisitiza mara kwa mara kuwa kituo cha Laikipia si mradi wa Amerika pekee, bali ni sehemu ya mpango mpana wa kujenga vituo 23 vya kutenga na kutibu wagonjwa wa Ebola nchini.

Hata hivyo, maelezo kuhusu vituo hivyo vingine bado hayajawekwa wazi. Serikali haijataja vinakojengwa, kaunti zinazohusika, hatua ya ujenzi wala muda wa kukamilika kwake.

Katika taarifa yake ya hivi karibuni, Bw Duale alisema serikali imeanzisha vituo maalumu vya Ebola katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta, Hospitali ya Kitaifa ya Polisi na Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Moi Eldoret, huku maeneo mengine zaidi ya 10 katika kaunti zilizo kwenye hatari kubwa yakitengwa kwa ajili ya kuimarisha maandalizi ya taifa.

Alisema mlipuko unaoendelea katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo unaonyesha kuwa magonjwa ya kuambukiza hayaheshimu mipaka na kwamba Kenya, kama kitovu cha biashara na usafiri, lazima iwe tayari kukabiliana na hatari hizo.

Serikali pia imesema inashirikiana na Amerika kujenga kituo kama hicho katika kambi ya kijeshi ya Laikipia ili kuimarisha ufuatiliaji wa magonjwa, uwezo wa kutenga wagonjwa na maandalizi ya dharura.

Lakini wataalamu wa afya wanahoji ikiwa maandalizi hayo yapo kwa vitendo.

Mtaalamu wa magonjwa ya kuambukiza, Profesa Shem Otoi, amesema serikali imekuwa ikiweka mkazo mkubwa kwenye kituo cha Laikipia huku ikikosa kueleza kuhusu vituo vingine 22.

“Serikali inasema inajenga vituo 23. Lakini viko wapi? Vinafikia hatua gani? Kaunti ziko tayari kweli?” alihoji.

Kwa mujibu wake, Mkenya wa kawaida hatatibiwa katika kituo cha Laikipia ambacho kinalindwa na jeshi na ambacho, kulingana na taarifa za Amerika, kinajengwa kwa ajili ya raia wa nchi hiyo wanaoweza kuathiriwa na Ebola.

“Ikiwa mvuvi wa Busia au mfanyabiashara wa Bungoma atapatikana na dalili za Ebola, hataenda Laikipia. Swali ni ataenda wapi?” aliuliza.

Profesa Otoi alitaja Hospitali ya Rufaa ya Alupe katika Kaunti ya Busia kama eneo lililotajwa kujengwa kituo cha kutenga wagonjwa lakini akasema hakuna maendeleo yanayoonekana.

“Kwa nini kituo cha Laikipia kinaendelea kujengwa hata baada ya mahakama kuamuru kisimamishwe ilhali vituo vingine vinavyopaswa kuwahudumia Wakenya havionyeshi hata msingi wa ujenzi?”

Chama cha Wanasheria nchini (LSK) pia kimeeleza mahakamani kuwa Kenya haina maabara ya kiwango cha juu ya kushughulikia virusi hatari kama Ebola na uzoefu wa kutosha wa kudhibiti mlipuko mkubwa wa ugonjwa huo.

Katibu Mkuu wa Chama cha Madaktari, Wafamasia na Madaktari wa Meno (KMPDU) Davji Atellah, amesema serikali inapaswa kutoa ushahidi wa miradi hiyo badala ya kutoa matangazo pekee.

“Tuonyesheni vituo hivyo. Tuambieni viko katika kaunti gani, ujenzi umefikia wapi na vitakamilika lini. Kutangaza si kujenga,” alisema.

Hata hivyo, huku serikali ikisisitiza kuwa Kenya iko tayari kukabiliana na Ebola, wadau wa afya wanataka uwazi zaidi kuhusu mahali vituo hivyo 22 vipo na kama kweli vinaendelea kujengwa ili kuhakikisha usalama wa wananchi.