BAJETI 2026: Serikali yasita kuanzisha ushuru mpya
Waziri wa Fedha John Mbadi alisema badala yake serikali itazingatia kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato na kupanua wigo wa walipa kodi bila kuwalemea wananchi.
Mbadi alisema ameamua kuepuka kuongeza mzigo kwa Wakenya wanaofanya kazi kwa bidii, huku akisisitiza umuhimu wa mageuzi katika mfumo wa ushuru ili kuhakikisha usawa na uwazi.
“Kwa makusudi, sijapendekeza ushuru mpya wala kuongeza viwango vya ushuru vitakavyowaongezea mzigo Wakenya.
Badala yake, tunalenga kuboresha ukusanyaji mapato, kuleta usawa katika mfumo wa ushuru na kuongeza idadi ya walipa ushuru bila kumlemea mwananchi,” alisema.
Alieleza kuwa kwa sasa ni Wakenya milioni 3.1 pekee wanaochangia ushuru kupitia mfumo wa Pay As You Earn (PAYE), ilhali mamilioni ya wengine wanaopata kipato hawachangii.
“Wengi wamekuwa wakijaza fomu za ushuru wakionyesha hawapati mapato kila mwaka. Hali hii lazima ibadilike,” aliongeza.