Akili MaliMakala

Zaidi ya mifugo milioni 10 wamechanjwa kupitia mradi wa kitaifa wa afya ya mifugo

Na SAMMY WAWERU June 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ZAIDI ya mifugo milioni 10 wamechanjwa kote nchini kupitia mpango wa kitaifa wa kuzuia magonjwa ya mifugo, Katibu katika Idara ya Maendeleo ya Mifugo, Jonathan Mueke amesema.

Akizungumza katika kongamano la African Food Fellowship (AFF) jijini Nairobi, Bw Mueke alisema mpango huo unaonyesha mwelekeo mpya wa Kenya katika kuimarisha mifumo ya kinga dhidi ya magonjwa ya mifugo na matumizi ya teknolojia katika usimamizi wa sekta hiyo.

Alisema zaidi ya wanyama milioni 10 katika kaunti 31 tayari wamechanjwa, huku serikali ikitumia mifumo ya kidijitali kama sajili za wakulima na majukwaa ya vocha za kielektroniki.

“Tunatoka katika mfumo wa kukabiliana na magonjwa baada ya kutokea na kuelekea katika kinga ya mapema inayolinda uzalishaji, masoko na mapato ya wafugaji,” alisema Bw Mueke.

Katibu katika Idara ya Maendeleo ya Mifugo, Jonathan Mueke akizungumza Jijini Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Serikali ya Kenya ilizindua rasmi mpango huo mapema Januari 2025. Aidha, unalenga kuchanja ng’ombe milioni 22 pamoja na kondoo na mbuzi milioni 50 katika kaunti zote 47 ili kudhibiti magonjwa kama Foot and Mouth Disease (FMD) na Peste des Petits Ruminants.

Katibu Mueke alisema licha ya ukosoaji kutoka kwa baadhi ya Wakenya, hasa kutoka kwa wanasiasa, mpango huo umeandikisha mafanikio makubwa. Alisema juhudi za chanjo zimeimarisha biashara ya mifugo na kupunguza hasara zinazotokana na magonjwa katika maeneo muhimu ya uzalishaji.

Aliongeza kuwa mpango huo umenufaisha zaidi maeneo Kame na Nusu-Kame (ASALs), ambayo yanashikilia kati ya asilimia 70 hadi 80 ya mifugo yote nchini. Maeneo hayo pia yanachangia zaidi ya asilimia 50 ya nyama inayoliwa nchini na kusaidia maisha ya zaidi ya watu milioni 10.

Katika kongamano AFF, African Food Fellowship ilielezea mchango wake katika kuimarisha uongozi na ubunifu katika mifumo ya chakula barani Afrika. Kiongozi wa shirika hilo nchini Kenya, Gacoki Kipruto alisema AFF inafanya kazi na karibu wadauhusika 500 wa mifumo ya chakula nchini Kenya, Rwanda na Zambia.

Baadhi ya kina katika jamii ya wafugaji Kajiado wakiangalia kondoo wao baada ya kupata chanjo. Picha|Sammy Waweru

“Vijana wengi sasa wanaingilia kilimo kupitia huduma, ubunifu na majukwaa ya kidijitali badala ya uzalishaji pekee,” akaambia Akilmali kwenye mahojiano ya kipekee. Pia, alieleza kuwa kundi la tano la wakulima litahitimu Julai mwaka huu. African Food Fellowship imekuwa ikiendesha mpango wa kufunza wakulima haswa jinsi ya kuboresha kilimo na biashara, huku ikilenga vijana.

Bw Mueke alisema ajenda ya serikali ya mageuzi kwenye kilimo nchini imeipa kipaumbele sekta ya mifugo, maziwa, nyama na Ngozi, pamoja na mazao kama mpunga, ngano, chai na kahawa. Aliongeza kuwa uzalishaji wa maziwa umefikia lita bilioni 5.4 huku mauzo ya nyama nje ya nchi yakiongezeka kufuatia kampeni za chanjo.