Jamvi La Siasa

KINAYA: Kaa rada usitumie akili zako kama kofia 2027

August 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HIVI ungali na akili zako au umeziangusha njiani? Adabu nazo umedumisha au umeziangika mahali ili kwanza uingie mjini kupambana na wanaume?

Siku tukimpenda Kasongo na UDA yake kama biriani, wapinzani wake walitubeza kwamba fuvu zetu zilikuwa ombwe.

Vibonzo vilichorwa kuonyesha vichwa vyetu vikiwa na mashimo makubwa yasiyokuwa na kitu.

Vingine vilionyesha watu wa Azimio wakiokota bongo zetu chini, kutuletea na kutwambia: “Shika, ubongo wako huu, nimeuokota chini.”

Nasi tukikataa na kusema: “Usiwe na hofu, sihitaji ubongo kamwe.”

Siasa zinaweza kukuvuruga kichwa ukabaki kujiuliza kama kweli unahitaji kufikiria, au uwaachie wanasiasa watumie akili zao, angalau weye zako zipumzike kidogo.

Ukizipumzisha tu, unachezwa shere na kubaki ukilia kwa miaka mitano ijayo au zaidi.

Baadhi ya wanoko wa Azimio walipitiliza unoko wao na kujifanya wanatusomea mistari fulani ya Biblia: “Waraka wa Mtume Paulo kwa watoto wa UDA… Hebu sikilizeni nyie watoto wa shetani…!”

Siasa zina vituko vyake, na lazima uwe mvumilivu wa kusikiliza maoni tofauti na yako, hata ikiwa yanasikika kama kelele za mwendawazimu sokoni.

Labda katika kelele hizo kuna cha kujifunza.

Nimekuuliza iwapo ungali na adabu kwa kuwa wakati mwingine mja hukataa kabisa kuwa mwema.

Nakumbuka enzi za makeke ya ujana tukitaniana kwamba sisi tuliotokea Mlima Kenya tuliangika adabu kwenye mti fulani mjini Ruiru kabla kuingia jiji kuu Nairobi.

Kisa na maana? Nairobi ni shamba la mawe, hakuna mama wa mtu, hivyo usitarajie kuhurumiwa au kusaidiwa na yeyote.

Maisha yakikushinda unarejea kwenu kijijini kula mahindi na maharagwe.

Leo sijui nikuandikie waraka, nikukumbushe kuwa na adabu kila wakati, au nikuhimize kutoangusha akili zao njiani.

Kuanzia leo, una mwaka mzima wa kuhitaji vitu hivyo vyote.

Naam, kuvihitaji hasa kwa kuwa wanasiasa wameanza kutembeza janja zao, kukukoroga akili na kukusihi uache kufikiria ili mtumie akili zao.

Eti zako si muhimu wakati huu wa kampeni za uchaguzi ujao.

Hofu yangu si janja za wanasiasa bali uwezo wako kutambua unapodanganywa na wajanja hao, na kutumia akili inavyostahili wala si kama kofia ya kukingia jua.

Sina shaka akili unazo nyingi. Nahofia tu kwamba unaweza kuamua kuzipumzisha utumie za wanasiasa.

Nahofia pia kuwa huenda ukakosa adabu na kufanya mambo ya kutia aibu ili uwafurahishe wanasiasa.

Kosa kubwa unaloweza kufanya ni kula hongo ili uchague mwizi, mshirikina, mcheza-kamari na watu wengine waovu kama hao.

Ol Kalou imetuonyesha kwamba tunaweza kula pesa za wezi na tukawanyima kura zetu.

– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)