Akili MaliMakala

Ufumaji vikapu kidijitali

Na SAMMY WAWERU June 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

UFUMAJI vikapu ni mojawapo ya shughuli za tangu jadi ambazo zimekuwa zikitekelezwa na kina mama, washirika wakitumia sanaa hiyo kujiingizia mapato.

Isitoshe, walithamini sana kuendeleza mila, itikadi na tamaduni za jamii huku ufumaji ukipitishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine.

Kuanzia nyanya za akina nyanya zetu, kina nyanya hao kupitisha biashara hiyo kwa kina mama zetu na katika baadhi ya maeneo ya Kenya na bara la Afrika, sasa ufumaji vikapu kizazi cha leo kikihamasishwa.

Turkana ni mojawapo ya kaunti ambazo utamaduni wa biashara ya vikapu bado inaendelezwa, na Ruth Acharait ni miongoni mwa kina mama ambao hii leo wangali wanaithamini.

Anahudumu chini ya kundi la Lodwar Baskets na pia ni mwanachama wa Beads Youth Group, makundi yaliyoanzishwa mwaka 2013 akiwa angali kijana.

Akijivunia kuwa na umri wa zaidi ya miongo mitano, Acharait pamoja na wanachama wenza hufuma vikapu lengo likiwa ni kujipa mapato, na, pia kuhakikisha utamaduni wa jamii kutoka Turkana unadumishwa.

“Ni biashara tuliyoirithi kutoka kwa kina mama zetu ambao pia walipokezwa na mama zao – nyanya zetu sasa,” anasema.

Muda unavyosonga na mambo kukua, ndivyo ufumaji vikapu pia unaimarika. Unakwenda na wakati.

Kulingana na Acharait, mjane ambaye ni mama wa watoto watatu awali vikapu vilikuwa vikifumwa kwa kutumia majani ya doum palm na papyrus reed grass huku vikirembeshwa kwa kutumia shanga – yaani beads.

Kikapu maridadi cheneye shanga kilichofumwa na Ruth Acharait kupitia muungano wa Lodwar Baskets, Turkana. Picha|Sammy Waweru

Mfumo wa soko ulikuwa ule wa kauli ya m ldomo kutoka boma moja hadi nyingine, au kwenye soko huru. Hata hivyo, ujio wa intaneti sasa umegeuza mbinu za uuzaji.

“Tunatumia safu za kidijitali kufikia wateja,” Acharait anaambia Akilimali. Majukwaa ya WhatsApp, Facebook, X (kitambo Twitter), Instagram na Tiktok, ndiyo safu za kisasa ambazo makundi ya Lodwar Baskets na Beads Youth Group yanatumia kufikia wateja.

Mfumo wa kiditali umesaidia makundi hayo kustawi ajabu. Umeandikisha ukuaji mara dufu. Beads Youth Group, kwa mfano, Acharait anadokeza kundi hilo 2013 lilianza na wanachama 10 na hii leo ni zaidi ya 20.

Kundi la vikapu, Lodwar Baskets, nalo limeandikisha maajabu ya ukuaji kiidadi. Kutoka kwa wanachama 5 waanzilishi, hii leo tunajivunia kuwa memba 47, Acharait akasema kwenye mahojiano ya kipekee na Akilimali.

“Kupitia intaneti na safu za kidijitali tumeweza kufikia wanunuzi si tu hapa nchini bali nje ya Kenya,” akaelezea. Hata ingawa hakufichua kiwango cha vikapu ambavyo kundi hilo hufuma kwa mwezi, kimafumbo alidokeza kwamba mauzo yamekua mara dufu.

“Tulipozindua makundi, kwa mfano, ikiwa tulikuwa tunauza vikapu 500 kwa mwezi, sasa idadi hiyo imekuwa mara dufu.” Ni ustawi unaotokana na kukumbatia teknolojia ya kisasa na mfumo wa dijitali.

Kila mama, anasema amejifunza kufanya mauzo mitandaoni kupitia unasaji wa video akifuma, kuhamasisha wateja na kuzipakia majukwaani.

“Ndio, miaka tunayo tumekula chumvi lakini tunakimbizana na vijana. Watoto wetu wametufunza kutumia safu za intaneti kuunda pesa kupitia bidhaa zetu,” anafafanua.

Ruth Acharait akikagua vikapu kwenye hafla ya World Vision jijini Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Ukuaji mwingine, kitambo walikuwa wakirembesha kwa shanga za rangi moja pekee ila sasa makundi hayo yamechanuka – yanajumuisha mseto wa rangi maridadi.

Cha kuvutia zaidi ni kwamba baadhi ya vikapu wanatia nembo ya bendera ya Kenya hatua ambayo inaiweka nchi kwenye ramani ya kimataifa.

Acharait alipoulizwa majukwaa mengine ya kijamii yakizinduliwa iwapo watayakumbatia, alijibu, “Huko ndiko ulimwengu unaelekea. Hata Rais wa sasa wa Kenya mwenyewe anahamasisha huduma za serikali ziwekwe kwenye safu za kidijitali, kwa nini sisi tusiende na wakati? Mitandaoni ndiko kila mmoja aliko.”

Makundi hayo yalikuwa miongoni mwa walionufaika kupitia mradi wa IMARA uliotekelezwa na World Vision Kenya kwa ushirikiano na Ubalozi wa Sweden, ukifikia watu 73,000 katika kaunti tisa kame na nusu-kame (ASAL), Turkana ikiwa mojawapo.

Kando na kufufuaardhi iliyoharibika na kuokoa miti katika maeneo lengwa, mpango huo wa miaka saba uliofadhiliwa na Serikali ya Sweden kupitia shirika la Swedish International Development Cooperation Agency (Sida) kwa gharama ya SEK211 milioni sawa na Sh3.22 bilioni – uliokamilika Aprili 2026, pia ulisaidia makundi ya kijamii yanayoendeleza biashara na kudumisha tamaduni za jamii.