Siasa

Kibarua kwa viongozi wa upinzani wakilenga kumng’oa Ruto 2027

Na BENSON MATHEKA June 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

VIONGOZI wa upinzani wanakabiliwa na presha kubwa kuthibitisha kwa vitendo umoja wao na uthabiti wa kisiasa kumpa Rais William Ruto ushindani mkali katika azma ya kutetea kiti chake.
Ingawa viongozi kutoka vyama mbalimbali vya upinzani wameendelea kuonyesha mshikamano dhidi ya serikali ya Kenya Kwanza, tofauti zinazojitokeza kuhusu uongozi, muundo wa muungano na namna ya kumpata mgombea mmoja wa urais zinaanza kufichua nyufa zinazoweza kuhatarisha umoja huo hata kabla haujaundwa rasmi.
Wadadisi wanasema changamoto kubwa inayokabili kundi hilo ni suala la nani atapeperusha bendera ya upinzani katika uchaguzi wa urais na ni utaratibu gani utakaotumika kumpata mgombea huyo.
“Kutoa Ruto jasho katika uchaguzi mkuu kutahitaji vinara wa upinzani kujitoa kafara na kuacha azma zao kuunga mmoja wao,” alisema mchambuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki.
Dalili za kwanza za mvutano zilijitokeza baada ya kiongozi wa People’s Liberation Party, Martha Karua, kupendekeza kuwa mgombea wa urais achaguliwe kupitia kura za maoni za kisayansi. Pendekezo hilo limeungwa mkono na mgombea urais wa Jubilee Fred Matiang’i ambaye anaamini tafiti za kitaalamu zinaweza kubaini mgombea mwenye nafasi kubwa ya kushinda.
Hata hivyo, washirika wa kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua wanaelekea kuunga mkono mfumo wa makubaliano ya kisiasa unaotegemea mashauriano, uzito wa kura za maeneo mbalimbali na maelewano ya ndani ya muungano badala ya kutegemea kura za maoni pekee.
Mitazamo hiyo tofauti imeonyesha ugumu unaowakabili viongozi wa upinzani wanapojaribu kuepuka migawanyiko ambayo imekuwa ikidhoofisha juhudi za kuondoa mamlakani serikali.
Hali imezidi kuwa tata kufuatia kuibuka kwa vuguvugu la Linda Mwananchi linalohusishwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo na baadhi ya viongozi kutoka ODM, Wiper na vyama vingine vinavyoshirikiana nao.
Ingawa pande zote mbili zinasisitiza kuwa bado zimejitolea kushirikiana pamoja dhidi ya Rais Ruto, watu wa karibu na mazungumzo hayo wanakiri kuwa bado hakuna mfumo rasmi wa kusimamia maslahi yanayokinzana, matarajio ya viongozi na tofauti za kiitikadi ndani ya upinzani mpana.
Kutokuwepo kwa muundo uliokubaliwa wa muungano pamoja na njia za wazi za kushughulikia masuala ya uongozi, kumezua wasiwasi miongoni mwa wafuasi wanaohofia kuwa ushindani wa ndani unaweza kuvuruga jitihada za kuunda kikosi chenye nguvu.
Uamuzi wa hivi karibuni wa Bw Gachagua kusitisha kushiriki mikutano ya kisiasa kwa siku 45 umeongeza suitafahamu katika mchakato wa kujenga muungano huo.
Baada ya Mahakama Kuu kuthibitisha kuondolewa kwake madarakani lakini pia kumpa fidia ya Sh50 milioni kwa kukiukwa haki yake ya kusikilizwa kwa haki, Gachagua alitangaza kuwa atajitenga nyumbani kwake Wamunyoro kufanya mashauriano ya kina na washirika wake wa kisiasa, wafuasi na viongozi wa maoni.
Alisema moja ya ajenda kuu katika mashauriano hayo ni kubuni mfumo wa kumpata mgombea mmoja wa urais wa upinzani chini ya mpango unaoitwa Serikali Mbadala ya Muungano.
Mashauriano hayo yanatarajiwa kujikita katika muundo wa uongozi, mikakati ya muungano na vigezo vitakavyotumika kumchagua mgombea atakayemkabili Rais Ruto mwaka 2027.
Hatua hiyo imejiri wakati ambapo shinikizo zinaongezeka ndani ya upinzani kutatua suala la tiketi ya pamoja kabla ya kampeni kuingia katika hatua ya juu.
Changamoto za ndani ya muungano zilianikwa hadharani wiki hii na msemaji wa Muungano wa Upinzani, Mukhisa Kituyi, aliyesema tamaa binafsi za kisiasa, ukosefu wa miundo madhubuti na ushindani ambao haujatatuliwa zinaweza kudhoofisha juhudi za upinzani.
Akizungumza katika mahojiano ya runinga ya humu nchini, Kituyi alisema viongozi wa upinzani wanakabiliwa na presha kubwa kutoka kwa wananchi kuhakikisha hakuna anayejiondoa mezani wakati wa mazungumzo ya kuunda muungano.
“Shinikizo kutoka kwa umma zinaongezeka kwamba hakuna anayepaswa kuondoka kwenye mazungumzo, lakini bado tunahitaji kujenga miundo itakayowaweka wadau wote pamoja,” alisema.
Kauli yake inaendana na onyo la awali kutoka kwa Naibu Kiongozi wa Jubilee Jeremiah Kioni ambaye mara kadhaa amesema upinzani bado uko katika mazingira hatari kwa sababu haujaunda mfumo rasmi unaobainisha uongozi, kanuni za uendeshaji na malengo ya kisiasa.
Kioni pia ameonya kuwa kuwepo kwa makundi yanayofanana kama Azimio na Muungano wa Upinzani kunaweza kuleta mkanganyiko na ushindani usio wa lazima.
Kwa mujibu wake, tofauti kati ya makundi yanayomuunga mkono Kalonzo na yale yanayomuunga mkono Gachagua bado hazijapatiwa suluhu na zinaweza kuathiri mazungumzo ya kuunda muungano ikiwa hazitashughulikiwa mapema.
Hatari ni kubwa zaidi ikizingatiwa kuwa Rais Ruto, kama rais aliye mamlakani, anatarajiwa kufaidika kwa nguvu za utawala katika harakati zake za kuwania muhula wa pili.
Kutokana na hali hiyo, viongozi wa upinzani wanalazimika kuonyesha sio tu umoja wa kisiasa bali pia nidhamu ya kiutawala na uwezo wa kujenga kampeni ya kitaifa yenye mshikamano na ufanisi wa kumshinda rais katika uchaguzi wa 2027.