Mke amegeuka DCI, anapekua simu na mifuko yangu kila nikiwasili nyumbani; nishauri
KILA ninaporudi nyumbani mke wangu hupenda kuangalia mfuko wangu, risiti nilizobeba na hata simu yangu. Anasema anafanya hivyo kwa sababu siku hizi watu wengi si waaminifu. Tatizo ni kuwa sijawahi kumpa sababu ya kunishuku. Sasa nahisi kama ninaishi na DCI. Nifanyeje bila kufanya mambo kuwa mabaya zaidi?
Uaminifu ni msingi wa ndoa. Ikiwa mwenzako anaishi kama mpelelezi na mwingine kama mshukiwa, amani hupotea polepole. Zungumza naye kwa utulivu kuhusu jinsi unavyochukizwa na hiyo tabia yake. Jaribu kuelewa pia chanzo cha hofu yake. Wakati mwingine mashaka hutokana na majeraha ya zamani au ukosefu wa usalama wa kihisia.
Mke ana tatizo la harufu kali na sijui nimuelezeje, naomba ushauri wako
KUNA jambo ambalo sijawahi kumwambia mtu yeyote. Mke wangu amekuwa na tatizo la harufu ya mwili kwa muda sasa. Najua anaoga na kujitunza, lakini wakati mwingine harufu huwa kali sana. Naogopa kulizungumzia kwa sababu sitaki kumuumiza hisia. Lakini kimya changu pia kinaathiri ukaribu wetu. Nifanyeje?
Mada kama hizi zinahitaji upendo, busara na heshima. Chagua muda mzuri wa kuzungumza naye faraghani na kwa lugha ya kujali. Usitumie maneno ya kumdhalilisha au kumlaumu. Wakati mwingine harufu ya mwili inaweza kuhusiana na afya, homoni au aina ya bidhaa zinazotumiwa. Mkaribie kama mke na rafiki anayejali ustawi wake, si mkosoaji. Mazungumzo ya heshima yanaweza kuleta suluhisho bila kuumiza uhusiano.
Mwanangu ni mtundu ajabu, imekuwa kesi baada ya kesi, sijui nitamdhibiti vipi
Shangazi, nina tatizo. Kila mara nina kesi kwa sababu ya mwanangu. Ana miaka 10 na amekuwa mkali sana na hupenda kupiga wenzake shuleni. Walimu wananilalamikia kila wiki. Sijui shida ni gani au kuna kitu kinamsumbua. Akienda shule, huwa najawa wasiwasi sana kwani kila simu kutoka shuleni ni malalamishi tu. Nimechoka sana. Nifanyeje?
Tabia ya ukali kwa watoto mara nyingi ni ishara ya kitu kilichofichika, labda ni huzuni, hasira au mazingira. Zungumza naye kwa upole na muulize kinachomsumbua au kumtatiza moyoni. Pia chunguza mazingira yake ya nyumbani na shuleni. Adhabu pekee haitoshi; anahitaji kuelekezwa namna ya kueleza hisia zake bila vurugu. Kumbuka kuwa usipoziba ukuta sahii, utajenga ukuta baadaye maishani.
Nakerwa na mume asiyependa kuoga
Nimeolewa kwa miaka sita na kuna jambo linalonitesa kimya kimya. Mume wangu ni mtu mzuri, anajali familia. Tatizo ni usafi wake binafsi. Mara nyingi hurudi kutoka kazini akinuka jasho lakini hataki kuoga. Wakati mwingine huenda kulala bila kuoga kabisa. Hali hii imeanza kuniathiri hasa katika ukaribu wa ndoa yetu kwa sababu sipati hamu ya kuwa karibu naye. Nikijaribu kumwambia, huona kama namdharau au kumkosoa. Nifanyeje bila kumuumiza hisia zake?
Usafi was kibinafsi si suala la anasa bali ni sehemu muhimu ya afya na mahusiano. Badala ya kumkosoa moja kwa moja, zungumza naye wakati mko katika hali nzuri na si wakati tatizo limetokea. Mweleze kuwa suala hili linakuathiri kihisia na hata ukaribu wa ndoa yenu. Tumia lugha ya upendo badala ya lawama. Wakati mwingine watu hawatambui jinsi tabia zao zinavyoathiri wenzao.