Kimataifa

Mswada wa kumpa Tshisekedi ‘Three Tam’ wapitishwa

Na REUTERS June 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KINSHASA, DR Congo:

SENETI ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Jumatano ilipitisha mswada wa kubadili katiba ambao una uwezo wa kumruhusu Rais Félix Tshisekedi kuhudumu kwa muhula wa tatu madarakani.

Hatua hiyo inajiri siku chache baada ya maandamano ya kupinga mswada huo kugeuka vurugu katika jiji kuu la Kinshasa.

Mswada huo unafungua njia ya kufanyika kwa kura ya maoni kuhusu katiba mpya.

Tshisekedi anahudumu muhula wake wa pili na wa mwisho kwa mujibu wa katiba ya sasa.

Maseneta 89 walishiriki katika kura hiyo iliyofanyika Jumatatu na wote walipiga kura kuunga mkono kupitishwa kwa mswada huo.

Maseneta 20 hawakushiriki katika upigaji kura.

Hata hivyo, mswada huo bado unahitaji kutiwa saini kuwa sheria na Rais Tshisekedi.

Seneta wa upinzani, Salomon Kalonda Della Idi, alisema katika taarifa kwamba mswada huo unaweza kusambaratisha nchi.

Wiki iliyopita, maandamano dhidi ya mswada huo yaligeuka vurugu wakati vikosi vya usalama vilipotumia vitoza machozi na kufyatua risasi hewani kuwatawanya waandamanaji.

Waliokuwa wakishiriki maandamano walirusha mawe, Wandani wa mwanasiasa wa upinzani Delly Sesanga walidai kupitia mtandao wa X kwamba alipigwa risasi mguuni wakati wa vurugu hizo.

Bunge la Kitaifa la DR Congo, ambalo ni bunge la chini, tayari lilikuwa limeidhinisha mswada huo kabla ya kupitishwa na Seneti.

Uchaguzi mkuu ujao wa urais DR Congo umepangwa kufanyika mnamo 2028.