Mkataba wa Sh1bn wa kukusanya ushuru wageuka jinamizi Kilifi
MWAKA wa 2014, kampuni ya Raindrops Limited ilitia saini mkataba wa thamani ya Sh1 bilioni na Serikali ya Kaunti ya Kilifi wa kukusanya mapato kwa kipindi cha miaka 15.
Mkataba huo ulitarajiwa kuongeza mapato ya kaunti hadi zaidi ya Sh700 milioni kwa mwaka na kukomesha ufisadi uliokuwa ukikumba idara ya ukusanyaji mapato.
Hata hivyo, zaidi ya miaka kumi baadaye, mkataba huo umegeuka kuwa mzigo mkubwa kwa kaunti hiyo, ambayo sasa inakabiliwa na hatari ya kulipa kampuni hiyo fidia ya Sh2.1 bilioni.
Katika uchunguzi wa Kamati ya Seneti ya Hesabu za Kaunti, ilibainika kuwa mkataba huo ulikuwa na dosari nyingi tangu mwanzo.
Waliotajwa kuhusishwa na mkataba huo ni Spika wa Seneti, Bw Amason Kingi, aliyekuwa gavana wa Kilifi wakati huo, na Mbunge wa Kilifi Kaskazini, Bw Owen Baya, aliyekuwa karani wa kaunti kati ya mwaka 2013 na 2017.
Gavana wa sasa wa Kilifi, Bw Gideon Mung’aro, aliambia kamati hiyo kwamba makosa yalifanywa tangu siku ya kwanza, ikiwemo kufunguliwa kwa akaunti maalum na kupatia kampuni asilimia kubwa mno ya mapato yaliyokusanywa.
Mkataba huo ulipatia Raindrops asilimia 30 ya mapato yote iliyokusanya, kiwango ambacho maseneta walikitaja kama cha kushangaza.
Kwa kulinganisha, Kaunti ya Mombasa ilikuwa ikilipa kampuni yake ya ukusanyaji mapato asilimia tano pekee.
Katika mwaka wa kifedha ulioishia Juni 2015, kampuni hiyo ilikusanya Sh545.5 milioni.
Kati ya fedha hizo, zaidi ya Sh136 milioni zilienda kwa kampuni hiyo, huku kaunti ikibaki na takriban Sh409 milioni, kiwango kilichokuwa chini ya mapato ya mwaka uliotangulia.
Mbali na kugharamia sehemu ya mapato, kaunti pia ilitakiwa kulipa mishahara ya wafanyakazi wa kampuni hiyo pamoja na ushuru mbalimbali.
Akaunti yake katika Benki ya SBM, iliyokuwa Chase Bank awali, iliruhusu kampuni kutoa fedha moja kwa moja kila mwezi.
Miezi michache baadaye, Bw Kingi aliyekuwa Gavana, alisitisha mkataba huo, hatua iliyosababisha Raindrops kuwasilisha kesi katika Mahakama Kuu ya Malindi mwaka 2015.
Tangu wakati huo, pande hizo zimekuwa katika vita vya kisheria vinavyohusisha pia Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC).
Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Bi Nancy Gathungu, ilibaini Sh44.35 milioni zilizolipwa kampuni hiyo bila vielelezo vya kutosha.
Fedha hizo zilikuwa zikikatwa moja kwa moja kutoka benki kwa kiwango cha Sh3.69 milioni kila mwezi.
Maseneta walishangazwa na jinsi kaunti ilivyoendelea kulipa fedha hizo kwa miaka mingi licha ya kutokuwa na ushahidi kuwa kampuni hiyo ilikuwa ikitoa huduma zinazostahili malipo hayo.
Aidha, umiliki wa Raindrops Limited umeibua maswali kwani taarifa za kampuni hiyo hazijathibitishwa katika sajili ya kampuni nchini.
Kamati ya Seneti sasa inaazimia kuwaita maafisa wa EACC pamoja na waliokuwa viongozi wa kaunti wakati mkataba huo ulipotiwa saini ili kueleza jinsi mabilioni ya pesa za umma zilivyotumika katika mpango huo unaotiliwa shaka.
Maseneta wameeleza kuwa waliohusika na kile walichokitaja kama “wizi mkubwa wa fedha za umma” lazima wawajibishwe ili kuzuia kashfa kama hiyo katika kaunti nyingine nchini.