Azma ya Taita Taveta kufaidi mapato ya Tsavo yagonga mwamba
GAVANA wa Kaunti ya Taita Taveta, Bw Andrew Mwadime, amefichua kuwa mapendekezo ya awali yaliyohitaji mapato kutoka mbuga ya kitaifa ya Tsavo yagawanywe kati ya serikali ya kitaifa na kaunti yalikwama, baada ya kubainika kwamba haikusanyi fedha za kutosha.
Akiondoa hofu ya umma kuhusu ujenzi wa ua katika hifadhi maalumu ya kifaru kwenye mbuga ya Tsavo Magharibi, Gavana Mwadime alisema mbuga hiyo ilikuwa ikitegemea ufadhili wa Wizara ya Fedha.
Viongozi wa eneo hilo wamekuwa wakishinikiza mapato ya Tsavo yagawanywe asilimia 50 kati ya serikali ya kitaifa na kaunti, na Rais William Ruto aliahidi kuhakikisha ombi lao linatimizwa.
Bw Mwadime alieleza matumaini yake kuhusu chanzo kingine cha mapato; malipo kutokana na usafishaji hewa kwa kuondoa gesi ya kaboni (carbon credits kwa Kimombo), kutoka mbuga ya Tsavo.
Sehemu kubwa ya hifadhi hiyo ya wanyamapori iko ndani ya Kaunti ya Taita Taveta.
Gavana alidokeza kwamba hivi karibuni alijadili suala hilo na Rais Ruto, kama chanzo mbadala cha mapato kwa kaunti yake.
Alisema utekelezaji wa mpango huo ukifaulu unaweza kufungua chanzo kipya cha mapato kwa kaunti, huku ukiimarisha juhudi za kuhifadhi mazingira na kukabili mabadiliko ya tabianchi.