Habari

Maandamano: Gavana Orengo sasa avaa kiatu cha Raila

Na CECIL ODONGO June 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

GAVANA wa Siaya, James Orengo, amejitokeza kama sura ya maasi dhidi ya serikali baada ya kifo cha Raila Odinga huku Wakenya wakiingia kwenye wiki ya kuadhimisha miaka miwili baada ya maandamano ya Gen Z mnamo 2024.

Maadhimisho hayo yatafanyika Alhamisi na Bw Orengo amekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha maandamano hayo yanafaulu.

Maadhimisho ya Juni 25 yamepangwa na familia, jamaa na marafiki wa wale waliouawa wakati wa maandamano ambayo yalifanya Bunge kuvamiwa mnamo Juni 25, 2024.

Maandamano hayo yalikuwa ya kupinga Mswada wa Fedha 2024.

Kwa mujibu wa Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu (KNCHR) idadi ya walioaga ilifika 60.

Wiki jana, Bw Orengo aliwaongoza wanasiasa Gitobu Imanyara, Martha Karua, aliyekuwa Jaji Mkuu Willy Mutunga pamoja na viongozi wengine kuwafahamisha polisi kuhusu maandamano ya Juni 25.

“Tunawaalika Wakenya wote kuandamana hadi majengo ya bunge kusaka haki na kuweka maua mahali ambapo watoto wetu walipigwa risasi hadi kufa,” akasema Bw Orengo.

“Utekaji nyara, mauaji yanayotekelezwa na polisi na mauaji ya kiholela bado yanaendelea ndio maana tuna maadhimisho ya Juni 25. Tumeambia serikali siku hiyo ni sikukuu ya kitaifa lakini bila ruhusa yao bado itakuwa sikukuu ya kitaifa,” akasema Bw Orengo.

Kiongozi huyo pia amepuuzilia mbali fidia ya Sh2 bilioni ambazo zilitangazwa na serikali wiki jana, akisema hela hizo ni dharau kwa sababu haziwezi kufufua waliouawa na polisi.

Bw Orengo akizungumza Kaunti ya Narok wikendi alisema utawala wa sasa unaelekea kuporomoka na sasa imejikita katika kukiuka haki za kibinadamu.

“Kuwa serikalini hakukusaidii chochote, lazima upiganie haki yako,” akasema Bw Orengo ambaye amejitangaza kiongozi wa ODM na pia vuguvugu la Linda Mwananchi.

Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa, Kimani Ichung’wah amemshutumu Bw Orengo kwa kuwaelekeza Wakenya vibaya akisema ni mkongwe ambaye anastahili kusaka suluhu kupitia mazungumzo kwa mambo anayopigania.

“Orengo anawaambia Wakenya waende wazue ghasia Nairobi. Nikiwa kijana katika Chuo Kikuu cha Nairobi, Orengo alikuwa akiandamana, sasa ana umri wa miaka 75 na bado anaandamana. Wakenya hawatapoteza maisha yao kutokana na siasa za watu kama Bw Orengo,” akasema Bw Ichung’wah.

Kuelekea maandamano ya Alhamisi, Rais William Ruto tayari ameonya wanaoyaratibu kuwa wasiingilie au kuvuruga biashara za watu wengine.
Kule Nyanza, viongozi wa ODM wamemwonya Bw Orengo kuwa apeleke maandamano maeneo mengine kwa sababu kujibwaga barabarani hakujawahi kusaidia eneo hilo kimaendeleo.

“Tunawaona wakongwe ambao walianza maandamano miaka ya 70 sasa ndio wanapanga maandamano na si Gen Z tena,” akasema Kiongozi wa wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohamed.

“Hapa Nyanza hatutaki maandamano na hatutaandamana. Tumeandamana miaka mingi na sasa ni zamu ya wengine kujaribu,” akasema Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga.