Isaac Ruto asema ana imani atashinda mchujo wa UDA kwa ugavana Bomet
ALIYEKUWA Gavana wa Bomet, Isaac Ruto, ametangaza kuwa ana imani atashinda uteuzi wa UDA na kurejelea kiti chake katika uchaguzi mkuu 2027.
Bw Ruto alisema kuwa uchaguzi wa mashinani wa chama hicho na matumizi ya vifaa vya kielektroni, ni baadhi ya masuala ambayo yamempa imani kuwa uteuzi huru utafanyika ndani ya UDA.
“UDA imeweka mikakati ya kuhakikisha kwamba uteuzi wa 2027 ni huru na wa haki na binafsi nikipoteza kwenye uteuzi, nitaridhika kuwa nimefanya hivyo kwa haki. UDA kwa sasa inafanya kazi kwa mtindo sawa na IEBC kwa sababu tuna vifaa ambavyo vitahakikisha kila mwaniaji anaridhika na matokeo ya mchujo,” akasema Bw Rutto kwenye mahojiano na Taifa Leo.
Kiongozi huyo alihudumu kama Gavana wa kwanza wa Bomet kati ya 2013-2017 ambapo alibwagwa 2017 na marehemu Joyce Laboso.
Katika uchaguzi huo, aliwania kupitia Chama cha Mashinani (CCM) huku marehemu Bi Laboso akigombea kupitia Jubilee.
Bw Ruto mnamo 2017 alimuunga mkono marehemu Raila Odinga huku wapigakura wa Bomet na Bonde la Ufa wakimpigia kura Uhuru Kenyatta.
Baada ya mauti ya Bi Laboso mnamo Julai 29, 2019, Naibu Gavana wakati huo, Hillary Barchok alichukua usukani na kwa sasa anahudumu muhula wake pili na wa mwisho.
Bw Rutto na Bw Barchok wapo kwenye muungano wa kisiasa ambapo Bw Rutto atagombea ugavana huku Bw Barchok akiendea useneta.
Gavana huyo alimshutumu Seneta wa sasa Hillary Sigei akisema ameshindwa kuwajibikia majukumu yake ipasavyo na anashiriki tu siasa za ukosoaji zisizokuwa na msingi.
Kiti cha useneta kinaonekana kumezewa mate na wanasiasa wengi Bomet akiwemo Chepkirui Kones, mwanawe mwanasiasa wa zamani marehemu Kipkalya Kones na mkewe Mbunge wa Belgut Nelson Koech.
Bw Ruto alisema malengo yake ni kuinua kilimo Bomet na kuhakikisha kuwa raia wa kawaida wananufaikia ugatuzi.
Pia amesema analenga kukamilisha baadhi ya miradi aliyoanzisha huku akisema kuwa ugatuzi licha ya kugubikwa na changamoto kadhaa, umesaidia maeneo mbalimbali kupiga hatua kimaendeleo.