Karua anyakwa na kuzuiliwa Uganda alikoenda kumwakilisha mwandani wa Besigye kortini
KIONGOZI wa PLP Martha Karua Jumatatu alizuiwa kuingia Uganda na kuamrishwa arejee Kenya, kwa mujibu wa Chama cha Mawakili Uganda (ULS).
Bi Karua alikuwa amesafiri Uganda kupitia ndege ya Kenya Airways pamoja na Rais wa Chama cha Mawakili Nchini (LSK) Charles Kanjama kuhudhuria kikao cha korti kwenye kesi ya Kiongozi wa Upinzani Uganda Kizza Besigye.
Bw Besigye amekuwa akizuiliwa baada ya kushtakiwa kwa kosa la uhaini na mawakili wake wakiongozwa na Bi Karua wamekuwa wakipambana ili aachiliwe kwa dhamana.
Bi Karua alikuwa ametua katika uwanja wa Entebbe kujiunga na wakili mwenzake Erias Lukwago, wote wakiwa mawakili wa Bw Besigye. Bw Lukwago mwenyewe alishtakiwa kwa makosa ya uhaini wiki jana na kesi yake ya kuachiliwa kwa dhamana ilikuwa isikizwe Jumatatu.
Serikali ya Uganda haikutoa sababu za kumzuia Bi Karua ingawa Bw Kanjama aliruhusiwa kuingia. Bw Kanjama mwenyewe alishangazwa na hatua hiyo akisema wote ni mawakili na walikuwa wameenda Uganda kwa kesi moja ya Bw Besigye.
“Ni vigumu kuelewa kwa nini mmoja wa mawakili anaruhusiwa na mwingine kuzuiwa,” akachapisha kwenye mtandao wa X huku akitaka maelezo kutoka kwa serikali ya Uganda.
Afisi ya Bi Martha Karua ilieleza kuwa juhudi zilikuwa zikiendelea kupata taarifa kutoka kwa Uganda kuhusu hatua hiyo na kurejea kwake Nairobi.
Bw Lukwago naye alifikishwa mahakamani Jumatano iliyopita akiwa dhaifu siku chache baada ya kukamatwa nyumbani kwake.
Alikana mashtaka ya kushindwa kuripoti kosa la uhaini linalohusiana na kesi ya Bw Besigye, na akaamriwa kusalia rumande gerezani akisubiri kusikilizwa kwa kesi hiyo.
Bw Besigye amekuwa kizuizini akikabiliwa na mashtaka ya uhaini tangu alipotekwa nyara Kenya na kurejeshwa kwa nguvu Uganda mwishoni mwa 2024.
Kutekwa kwake, pamoja na kwa msaidizi wake Obeid Lutale, kulizua mjadala mkali katika eneo la Afrika Mashariki kuhusu mamlaka ya kisheria na masuala ya haki za binadamu.
Bi Karua alikumbana na vikwazo kadhaa kabla ya kuruhusiwa rasmi kumwakilisha Bw Besigye mahakamani. Miongoni mwa changamoto hizo ni ombi lake la awali la kuruhusiwa kufanya kazi ya uwakili nchini Uganda kukataliwa.
Aidha, mwaka jana alifurushwa Tanzania ili kumzuia kuhudhuria kesi ya kiongozi wa upinzani Tundu Lissu, ambaye pia anakabiliwa na mashtaka ya uhaini.