Habari za Kitaifa

Gachagua akubali fidia ya Sh50m, akata rufaa kwa maamuzi mengine ya korti

Na CECIL ODONGO, JOSEPH WANGUI June 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua Jumanne alikubali fidia ya Sh50 milioni kwa kutimuliwa serikalini bila kusikizwa, lakini akakata rufaa kuhusu maamuzi mengine yote yaliyofanywa na mahakama.

Bw Gachagua aliwasilisha notisi ya rufaa ya kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu ambao ulidumisha kutimuliwa kwake kama naibu rais mnamo 2024.

Kwenye rufaa yake, anapinga sehemu kubwa ya uamuzi huo lakini hajakata rufaa kuhusu uamuzi wa kulipwa Sh50 milioni kutokana na haki yake ya kusikizwa kukiukwa. Mahakama iliamrisha alipwe Sh50 milioni kwa sababu haki zake za kikatiba zilikiukwa.

Hatua yake ya kutokata rufaa kuhusu uamuzi wa kulipwa Sh50 milioni inatarajiwa kuzua ubabe mkali wa kisheria kati ya mawakili wake na wale wa serikali katika Mahakama ya Rufaa.

Kwenye uamuzi uliotolewa Juni 8, Mahakama Kuu ilibaini kuwa maseneta walivunja haki yake ya kusikizwa kwa kukataa kusitisha vikao wakati alikuwa akiugua.

Ingawa hivyo, jopo la majaji watatu Eric Ogolla, Antony Mrima na Frida Mugambi lilisema kukiukwa kwa haki hiyo hakuwezi kutumiwa kuharamisha kutimuliwa kwake.

Pia majaji hao walisema kuwa kumrejesha madarakani kungesababisha kuwe na manaibu rais wawili jambo ambalo haliwezani kisheria.

Jopo hilo lilikataa hoja nyingi zilizowasilishwa na Bw Gachagua pamoja na walalamishi wenzake.

Badala yake, mahakama iliidhinisha uamuzi wa Bunge wa kumuondoa afisini na kupisha mrithi wake, Profesa Kithure Kindiki, kuendelea kuhudumu kama Naibu Rais.

Majaji hao walibainisha masuala saba muhimu ya kuamuliwa iwapo maombi hayo yalikuwa yanastahili kusikilizwa mahakamani na iwapo mchakato wa kumtimua ulikuwa umefuata sheria.

Hasa walitaka kujua iwapo kulikuwa na ushirikishaji wa kutosha wa umma.

Masuala mengine yalihusu iwapo kanuni za Bunge zilizopingwa zilikuwa za kikatiba, iwapo taratibu za kikatiba zinazohusu kutimuliwa na za urithi wa uongozi zilifuatwa na iwapo Bw Gachagua alipatiwa haki ya kusikizwa.

Moja ya hoja kuu za Bw Gachagua ilikuwa kwamba wabunge na maseneta walikuwa tayari wameamua matokeo ya mchakato wa kumtimua kabla ya kuusikiliza.

Mahakama ilisema kuwa hakuna ushahidi wa moja kwa moja uliowasilishwa kuthibitisha madai hayo.

Majaji pia waliamua kuwa Seneti haikulazimika kufanya zoezi tofauti la ushirikishaji wa umma kwa sababu jukumu lake katika mchakato wa kumbandua Bw Gachagua lilikuwa la kutoa uamuzi wa kisheria na si kutunga sheria.

Vilevile, mahakama ilikataa hoja kwamba ushirikishaji wa umma ulikuwa muhimu katika uteuzi na kuidhinishwa kwa Profesa Kindiki kuwa Naibu Rais.