Mtindo mpya wa wanawake kuvalia pete ‘kufukuza wanaume wasumbufu’
WANAWAKE wengi wasio na waume nchini Kenya wameibuka na mbinu mpya ya kujikinga dhidi ya usumbufu wa wanaume wanaowafuatilia kimapenzi bila ridhaa yao kwa kuvalia pete zinazofanana na za uchumba au ndoa.
Ingawa pete hizo kwa kawaida huashiria kuwa mtu ameolewa au amechumbiwa, baadhi ya wanawake wanasema wanazivalia ili kuweka mipaka na kupunguza usumbufu unaotokana na wanaume wanaowanyemelea mara kwa mara.
Nancy Wachira, mkazi wa Kisiwa cha Lamu, ni miongoni mwa wanawake hao. Anasema amekuwa akivalia pete ya aina hiyo tangu Januari mwaka huu ili kuzuia wanaume wanaomtamani na ambao yeye hawataki.
“Mimi ni mseja lakini nimekuwa nikivalia pete hii kwa miezi kadhaa. Sababu kuu ni kujiepusha na usumbufu usio wa lazima kutoka kwa wanaume,” alisema.
Kulingana naye, wanawake wengi wanaofanya kazi hukumbana na changamoto ya kukosa kuheshimiwa na baadhi ya wanaume ambao hujaribu kuanzisha mahusiano ya kimapenzi hata mahali pa kazi.
“Pete imenisaidia sana. Wanaume wengi wanapoiona hudhani nimeolewa na hujihadhari. Hilo limenipa nafasi ya kuzingatia kazi na malengo yangu bila bughudha nyingi,” alisema.
Nancy anasema amenunua pete kadhaa, baadhi zikiwa na thamani ya kati ya Sh5,000 na Sh40,000. Pete yake ya sasa ya fedha safi iligharimu Sh15,000.
Hata hivyo, anasema kuvalia pete hiyo hakumaanishi kwamba amefunga mlango wa mapenzi.
“Bado niko wazi kwa ndoa. Kuna wanaume jasiri ambao hawashtushwi na pete na bado hujitokeza. Nikimpata mtu anayenivutia na mwenye sifa ninazotafuta kwa mwenzi wa maisha, sitakuwa na shida kuiondoa pete hiyo,” alisema.
Sabrina Mkare Jefwa, mwenye umri wa miaka 25, pia amekumbatia mbinu hiyo.
Sabrina huvalia pete inayofanana na ya uchumba ambayo alinunua kwa Sh35,000. Anasema lengo lake ni kuwafanya wanaume wanaotaka kumfuatilia wafikirie mara mbili kabla ya kumkaribia.
“Ninatarajia kuolewa siku moja iwapo Mungu atapenda, lakini kwa sasa nina mambo mengi ya kuzingatia maishani. Sitaki usumbufu wa mara kwa mara kutoka kwa wanaume,” alisema.
Kwa mujibu wake, mbinu hiyo imekuwa na mafanikio kwa kiasi kikubwa.
Naye Mercy Kahindi, mwalimu wa miaka 33 kutoka Malindi, anasema amekuwa akivalia pete ya ndoa bandia kwa zaidi ya miaka mitatu.
Anasema katika jamii yake ya Wamijikenda, wanawake wengi hukabiliwa na shinikizo la kuolewa wanapofikisha umri wa miaka 25.
Hata hivyo, wataalamu wana maoni tofauti kuhusu mtindo huo.
Mwenyekiti wa Chama cha Ushauri wa Kisaikolojia Kenya tawi la Lamu, Andrew Masama, anasema pete ya ndoa au uchumba inaweza kuwa na athari tofauti kwa watu wanaoiangalia.
Anaeleza kuwa baadhi ya watu huona pete hiyo kama ishara kwamba aliyeivalia ni mtu mwaminifu, mwenye uwezo wa kujitolea katika uhusiano na anayefaa kuwa mwenzi wa maisha.
“Wakati wengine wataheshimu mipaka hiyo na kuamua kutomkaribia mwanamke mwenye pete, wengine wanaweza kuvutiwa zaidi kwa sababu wanaamini tayari amethibitishwa kuwa mwenzi bora,” alisema.
Masama alionya kuwa ingawa pete inaweza kuwazuia wanaume wanaotafuta mahusiano ya muda mfupi, inaweza pia kuwafukuza wachumba wa kweli.
“Watu wengi huamini mwanamke akifika umri huo anapaswa kuwa ameolewa. Pete hii imenisaidia kuepuka maswali mengi na usumbufu kutoka kwa wanaume,” alisema.
Mercy anasema anatarajia kuacha kuvalia pete hiyo atakapofikisha miaka 35 ili kuwapa nafasi wanaume wanaoweza kuwa wachumba wa kweli kumkaribia.
Kwa upande wake, Eunice Wangari wa Mpeketoni amesema kuvalia pete hiyo kumemsaidia kujidhibiti baada ya kupitia mahusiano kadhaa yaliyomvunja moyo.
“Nilikuwa nakutana na wanaume waliodai wanataka ndoa lakini baadaye walikuwa na nia tofauti. Pete imenisaidia kupunguza majaribu hayo na kunipa amani ya akili,” alisema.
Kwa upande mwingine, mshauri wa ndoa na familia Hindu Salim anaunga mkono hatua ya wanawake hao.
“Ikiwa kuvalia pete kutawasaidia wanawake kuepuka mahusiano yasiyofaa au ngono kabla ya ndoa, basi ni jambo la kupongezwa. Wanawake hao wanajua wanachotaka na wakimpata mtu sahihi hawatasita kuondoa pete hizo,” alisema.