Nisaidieni kunasua ndugu zangu dhehebu la babangu, mwanawe Mackenzie alilia korti
MWANA wa mshukiwa wa mauaji ya Shakahola Paul Mackenzie, ameambia mahakama yuko tayari kutoa ushuhuda kuhusu dhehebu lililoongozwa na babake, akieleza masikitiko kwamba ushawishi wa dhehebu hilo bado umekita mizizi katika familia yao.
Kulingana naye, ndugu na jamaa zake wanaoishi katika boma lao neo la Furunzi viungani mwa Malindi, Kaunti ya Kilifi, bado wanaishi chini ya mafundisho ya kupotosha ya kidini.
Wakati wa ziara ya mahakama katika boma lao, Bw Dan Mackenzie, alisema ndugu zake wadogo bado wameathirika kwani wangali wanafuata mafundisho potovu, ikiwemo kutoenda shuleni na kukataa kutumia matibabu wanapougua.
“Ni kama utumwa wa kiakili. Watoto hawa bado wako katika dhehebu hilo,” alisema.
Aliiambia mahakama kwamba juhudi kuwaokoa watoto hao hazijazaa matunda.
“Naomba mahakama iingilie kati na Idara ya Huduma za Watoto iwachukue na kuwaokoa,” alisema.
Dan pia alieleza kuwa maisha ya ndugu zake wadogo yamebadilika kabisa tangu baba yao pamoja na mama yao Rhoda Mumbua Maweu walipokamatwa.
Aidha, aliomba kesi hiyo iharakishwe kusikilizwa, akisema familia imekumbwa na changamoto kubwa tangu kukamatwa kwa baba yake.
Alithibitisha kwamba makazi hayo yalikuwa nyumba ya baba yake na pia kituo cha kupokea wageni kabla ya Mackenzie na baadhi ya wafuasi wake kuhamia msituni Shakahola.
“Tulikuwa tunaishi hapa kabla baba yangu na ndugu zangu hawajaondoka kwenda Shakahola. Mimi sikwenda nao,” alisema.
Jaji wa Mahakama Kuu, Bi Wendy Kagendo, aliagiza mchakato wa kuwaokoa watoto hao uanzishwe wiki hii.
Dan aliieleza mahakama kuwa yuko tayari kutoa ushahidi zaidi kuhusu madai ya itikadi kali inayoendelea katika nyumba hiyo ya baba yake.
Mackenzie alirejea katika kanisa na boma lake kwa mara ya kwanza baada ya kuzuiliwa gerezani kwa takriban miaka mitatu kufuatia kukamatwa kwake mwaka 2023 kuhusiana na mauaji ya halaiki ya Shakahola.
Ziara hiyo ilikuwa sehemu ya ukaguzi wa maeneo mbalimbali yanayohusishwa na kesi ya uhalifu dhidi ya ubinadamu inayomkabili Mackenzie pamoja na washtakiwa wenzake.
Kituo cha kwanza cha msafara huo kilikuwa katika kanisa la Good News International Church, ambako Mackenzie alikuwa akihubiri awali.
Akiwa ameandamana na mawakili, waendesha mashtaka, maafisa wa upelelezi na jaji anayesikiliza kesi hiyo, Mackenzie aliingizwa ndani ya jengo hilo huku mahakama ikisikiliza maelezo kuhusu shughuli zilizokuwa zikifanyika hapo kabla ya tukio la Shakahola.
Mahakama ilielezwa kuwa kanisa hilo lina uwezo wa kubeba waumini wapatao 1,500 kwa wakati mmoja na kwamba ndilo lilikuwa kitovu cha mafundisho yaliyowavutia mamia ya wafuasi kutoka maeneo mbalimbali nchini.
Baada ya ukaguzi wa kanisa kukamilika, ndipo msafara huo ulielekea katika makazi ya Mackenzie yaliyo Furunzi ambapo mama yake pamoja na baadhi ya watoto wake wanaishi.
Mamake Mackenzie alipata fursa ya kuzungumza kwa kifupi na mahakama. Alisema hana pingamizi na shughuli inayofanywa na mahakama na kwamba anaelewa sababu za ziara hiyo.
Hata hivyo, licha ya uwepo wa mwanawe, hakuruhusiwa kumsalimia wala kuzungumza naye wakati wote wa shughuli hiyo.
Kutoka nyumbani kwa Mackenzie, msafara huo ulielekea katika majengo na nyumba mbalimbali ambazo, kwa mujibu wa ushahidi uliowasilishwa mahakamani, zilitumika kuwaweka wafuasi wa kanisa hilo kwa muda kabla ya kuhamishwa hadi katika msitu wa Shakahola.
Mahakama ilielezwa kuwa baadhi ya waumini walikuwa wakikusanywa katika maeneo hayo kabla ya kusafirishwa kwa makundi kuelekea msituni, ambako wengi wao walifunga kula kwa muda mrefu hadi kufariki dunia kwa njaa na kiu.