Gavana Wanga achemsha maseneta kwa matumizi ya Sh500,000 kujenga choo
GAVANA wa Homa Bay Gladys Wanga alipofika mbele ya Kamati ya Seneti ya Hesabu za Umma wiki iliyopita kujibu hoja zilizotolewa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhusu matumizi ya fedha katika mwaka wa kifedha wa 2024/2025, moja ya mambo yaliyozua mjadala mkubwa ni matumizi ya Sh500,000 kujenga choo cha mashimo chenye milango miwili katika ufuo mmoja wa eneo la Suba Kusini.
Kwa zaidi ya wiki moja sasa, suala hilo limekuwa gumzo kuu katika mitandao ya kijamii na mikusanyiko ya wananchi huku wakazi wakijaribu kubaini gharama halisi ya kujenga choo cha mashimo.
Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna alizua hoja hiyo aliporejelea madeni ambayo bado hayajalipwa, akitaja mradi wa choo katika Ufuo wa Ngeri, Kaksingri Magharibi, ambao ulikuwa umekamilika na kukabidhiwa lakini haujalipwa. Gharama ya mradi huo ni Sh348,954.
“Je, ina maana vyoo ni ghali kiasi hicho kujengwa Homa Bay?” alihoji Bw Sifuna.
Akijibu mbele ya Seneti, Bi Wanga alisema hicho ndicho kiwango cha kawaida kinachotumika kujenga choo cha mashimo chenye milango miwili.
“Hiyo ndiyo gharama ya kuchimba na kujenga choo hicho. Mara nyingi huwa karibu shilingi milioni,” alisema.
“Gharama hutegemea eneo unalojenga na muundo wa udongo. Mtu mwingine anaweza kutoa bei ya chini zaidi,” gavana aliwaambia maseneta.
Kutokana na ukosoaji huo, maafisa wa kaunti wamekuwa wakijitahidi kueleza kwa kina jinsi fedha hizo zinavyotumika.
Wakati wa ibada katika Kanisa la Roho eneo la Ugina, Mfangano, Jumapili iliyopita, Afisa Mkuu wa Elimu, Bw Martin Opere, alitetea matumizi hayo na kueleza sababu ya gharama hiyo.
Alisema mchakato wa ujenzi wa miradi ya serikali huanza kwa kutangazwa kwa zabuni ambapo kampuni mbalimbali huwasilisha maombi yao.
Wataalamu wa ujenzi pia wameeleza kuwa gharama ya miradi hutegemea hali ya eneo husika, ikiwemo uimara wa udongo, mazingira na upatikanaji wa eneo la mradi.
Mwenyekiti wa Chama cha Wakandarasi na Wasambazaji wa Homa Bay, Collins Omito, alisema maeneo yenye udongo dhaifu huhitaji msingi wa gharama kubwa unaoweza kuchukua kati ya asilimia 30 na 40 ya gharama yote ya ujenzi.
Alisema hali hiyo huongeza gharama kutokana na hitaji la uchimbaji wa kina, matumizi ya vyuma vingi vya kuimarisha msingi na ujenzi wa sakafu imara.
“Ukijumlisha ushuru, faida ya mkandarasi na gharama nyingine, ujenzi wa choo cha milango miwili unaweza kuzidi Sh500,000 katika eneo lenye udongo dhaifu. Kiwango kilichotajwa na gavana kinaweza kuwa sahihi,” alisema.