Baba asimulia jinsi bintiye mwislamu alibadilisha dini akayoyomea msituni kwa Mackenzie
MWANAMUME ameeleza mahakama jinsi binti yake alivyoingia kwenye uhusiano wa kimapenzi na mhudumu wa tuk tuk, akabadilisha dini kutoka Uislamu hadi Ukristo, kisha akatoweka msituni Shakahola.
Bw Hamisi Abdalla Mohamed, alifichulia mahakama jinsi alivyomwajiri Julius Thuva Luwali awe akisafirisha mboga kutoka nyumbani kwake Sabaki kwenda Soko la Malindi, kabla kumwoa binti yake, Nuru Hamisi, na hatimaye kumuingiza katika dhehebu la mhubiri Paul Mackenzie, ambako alitoweka bila kujulikana alipo hadi leo.
Bw Mohamed alikuwa amemfahamu Thuva kwa karibu miaka miwili na mara kwa mara alimwajiri kusafirisha mazao yake.
“Ningempigia simu kisha aje nyumbani kwangu na kusafirisha bidhaa kwa malipo kwa kutumia tuk tuk yake,” aliiambia Mahakama Kuu ya Malindi.
Kutokana na ziara zake za mara kwa mara, Thuva alizoeana na familia hiyo.
Nuru alipofikia utu uzima na baba yake akijiandaa kumpeleka kuendelea na masomo, aliwaambia jamaa zake kwamba alikuwa amepata kazi katika hoteli mjini Malindi.
Hata hivyo, tabia yake ilianza kubadilika na mara kwa mara alikosa kurejea nyumbani, akieleza kuwa alikuwa analazimika kulala kwa rafiki yake wa kike kutokana na majukumu ya kazi.
“Siku moja nilishikwa na hasira kwa sababu ya mienendo hii na nilipomhoji, aliniambia alikuwa akikaa nyumbani kwa Thuva kwa sababu walitaka kuoana,” Bw Mohamed aliambia mahakamani, mapema wiki hii.
Alisema alimweleza binti yake kwamba Thuva alipaswa kubadilisha dini kabla ya kufunga ndoa naye.
Hata hivyo, kufikia wakati huo Nuru alikuwa tayari ameukumbatia Ukristo na kuwa mfuasi wa kanisa la Mackenzie na baadaye akafunga ndoa na Thuva.
Jitihada za Mohamed kuleta uhusiano mwema kati ya familia hizo mbili hazikufanikiwa.
Nuru alianza kujitenga zaidi na familia yake, akitembelea nyumbani mara chache na kutojibu simu.
Familia ilikuja kufahamu kuwa yeye na Thuva walikuwa wamepata watoto wawili na kuhamia Witu, Kaunti ya Lamu.
Bw Mohamed alisisitiza kwamba hakupinga mazungumzo ya mahari, bali alitaka ndoa hiyo ifanywe kwa mujibu wa sheria za Kiislamu.
Kufikia mwaka 2022, Nuru hakuweza kupatikana. Ripoti zilipoibuka mapema mwaka wa 2023 kwamba wafuasi wa Mackenzie walikuwa wakifunga hadi kufa, Bw Mohamed alihofia kwamba binti yake na mkwe wake walihusika.
Hofu hizo ziliongezeka baada ya kuarifiwa kwamba wote wawili walikuwa wametoweka.
Sampuli za DNA walizotoa baada ya mkasa wa Shakahola hazikutoa matokeo yoyote kufikia sasa.
“Namchukia Thuva kwa sababu yeye yuko hapa hai ilhali binti yangu hajulikani aliko. Nataka aniambia binti yangu yuko wapi na jinsi ninavyoweza kumpata,” aliiambia mahakama.
Nuru, mtoto wa pili katika familia yenye watoto 10, bado hajapatikana huku baba yake akiendelea kutafuta majibu kuhusu hatima ya binti ambaye anaamini alipotea kwanza kupitia uhusiano wa kimapenzi, kisha mabadiliko ya dini, na hatimaye kupitia harakati iliyohusishwa na moja ya majanga mabaya zaidi ya madhehebu nchini.