Siasa

Junet, Wanjala wampigia debe Oparanya awe mgombea mwenza wa Ruto

Na DOMNIC OMBOK June 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

ODM sasa inaonekana kukumbatia mikakati ya kutaka nafasi ya mgombeaji mwenza ili kuimarisha ushawishi wake kuelekea mazungumzo na UDA kuhusu kura ya 2027.

Wikendi baadhi ya wabunge walisema Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya anatosha kuwa mgombea mwenza wa Rais William Ruto katika uchaguzi mkuu wa 2027.

Wabunge hao walisema kwamba yalikuwa mapenzi ya marehemu Raila Odinga mgombea mwenza wa Ruto atoke Magharibi mwa nchi na pia awe mwanachama wa ODM.

“Tulikutana kama viongozi wa Magharibi na tukaamua wakati umefika wa kuwa na mgombeaji mwenza wa urais kutoka eneo hili. Oparanya ndiye kiongozi tunayempigia upatu,” akasema Mbunge wa Budalang’i Raphael Wanjala.

Alikuwa akiongea katika mkutano wa kisiasa mjini Busia ambao ulihudhuriwa na vigogo wengine wa chama.

Kauli yake inajiri baada ya baadhi ya wabunge wa ODM kutoka kanda ya Pwani kumpigia debe Waziri wa Madini Hassan Joho awe mgombea mwenza wa Rais.

Nao wenzao kutoka Nyanza wamekuwa wakimsihi Ruto amchague Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga, licha yake kutangaza kwamba atawania muhula wa pili wa ugavana.

Viongozi wa mrengo wa serikali wanaoegemea Kenya Kwanza, hasa chama cha Ford Kenya, nao wamekuwa wakirindima ngoma ya Spika wa Bunge Kitaifa Moses Wetang’ula kuwa mgombe mwenza wa Ruto wakisema chaguo lake litamuandalia njia ya kukwea ngazi ya urais 2032.