Habari za Kitaifa

Wabunge waeleza wasiwasi wa Nyumba Nafuu kukwama licha ya mabilioni kukusanywa

Na SAMWEL OWINO June 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WABUNGE wameelezea wasiwasi wao kufuatia kusimama kwa miradi ya ujenzi wa nyumba za bei nafuu, licha ya serikali kuendelea kukusanya mabilioni ya pesa kila mwezi kutoka kwa wafanyakazi kupitia ushuru wa nyumba.

Wanahoji kuwa pesa zinaendelea kukatwa kwenye mishahara ilhali katika maeneo mbalimbali nchini wanakandarasi wameingia mitini wakidai hawajalipwa.

Sasa baadhi wameeleza hofu kuwa mpango huo, ambao ni kati ya ajenda kuu za utawala wa Rais William Ruto, utasambaratika.

Waziri wa Ardhi Alice Wahome pamoja na Katibu wa Wizara Charles Hinga wametakiwa kufika katika kikao cha dharura – maarufu kamukunji – siku ya Alhamisi kueleza zilikoenda pesa za kutekeleza ujenzi wa nyumba hizo nafuu.

Mbunge wa Sotik Francis Sigei aliibua suala hilo bungeni akisema licha ya eneobunge lake kutambuliwa kuwa miongoni mwa yale yaliyonufaika na ujenzi wa nyumba 596, hakuna kinachoendelea.

Bw Sigei alihoji kuwa mwanakandarasi wa ujenzi wa nyumba hizo Sotik aliacha kazi sababu ya kutolipwa.

Alidai mkandarasi huyo alivunja mkataba kwa madai kwamba ulikiukwa.

“Kuchelewa huku kumewanyima wakazi wa eneobunge la Sotik manufaa yanayotokana na mradi, na pia kunazua maswali kwani atalipwa fidia kwa mkataba wake kutoheshimiwa,” akasema Bw Sigei.

Maelezo ya kina

Mwanasiasa huyo anataka maelezo ya kina kuhusu lini ujenzi huo utarejelewa kwani amethibitisha mwanakandarasi alishaondoka.

Mbunge wa Turkana ya Kati Joseph Emathe naye alishangaa kwa nini miradi inasimama ilhali fedha zipo.

“Kuna fedha za ushuru wa nyumba ambazo zinakatwa. Kwa nini malipo yanachelewesha? Wanakandarasi walipwe kwani makato yanawasilishwa kila mwezi,” akaongeza.

Mbunge wa Igembe ya Kati Daniel Karitho naye alifichua kuwa ujenzi wa nyumba hizo ulisitishwa katika eneobunge lake miezi minne iliyopita.

“Katika eneobunge langu mwanakandarasi alifika, akachimba mitaro michache kisha akaondoka. Huu ni mradi muhimu sana kwa sababu hata Rais mwenyewe amekuwa akizunguka akiuzungumzia. Fedha zipo, tunataka kuona kazi ikiendelea,” akahoji.

Mbunge wa Eldas Adan Keynan alisema wizara inapaswa kueleza wazi fedha zinazokusanywa kupitia ushuru wa nyumba zimeelekezwa wapi.

“Miradi hii ilipozinduliwa tulifurahi sote, lakini sasa imesimama. Ushuru huu uko wapi? Fedha ziko wapi? Kwa nini miradi ilianzishwa halafu ikasimama? Itakuwa aibu ikiwa miradi inayofadhiliwa kupitia ushuru itakwama,” aliongeza Bw Keynan.

Mbunge wa Marakwet Mashariki Kangogo Bowen pia alisema hakuna shughuli za ujenzi ambazo zimefanyika eneo lake kwa miaka miwili.

Serikali inatarajia kukusanya takriban Sh500 bilioni katika kipindi cha miaka mitano kupitia ushuru wa nyumba, ili kufadhili ujenzi wa makazi hayo nafuu na kuimarisha miundomsingi nchini.