Makosa katika kukanusha sentensi za wingi, ngeli ya ‘I-ZI’ hali tegemezi
HALI tegemezi ‘nge’ – na ‘ngali’- hutumiwa kutunga sentensi zinazoashiria kuwa kitendo cha pili hakikufaulu kwa sababu kitendo cha kwanza kilikosa kufaulu au kilikosa kutendeka.
Kufaulu kwa kitendo cha pili hutegemea kufaulu kwa kitendo cha kwanza.
Tunapokanusha sentensi katika hali tegemezi ‘nge’- na ‘ngali’ huwa tunatumia ‘singe’ na ‘singali’ mtawalia.
Iwapo kukanusha sentensi katika hali tegemeze ‘nge’- na ‘ngali’ ni rahisi, kuna baadhi ya wanafunzi ambao hukumbwa na changamoto wanapokanusha sentensi zilizotungwa kwa kutumia nomino za wingi ngeli ya I-ZI.
Baadhi ya wanafunzi hukosa kutofautisha kiambishi cha uwiano wa kisarufi katika wingi wa ngeli ya I-ZI na kiambishi cha ukanusho wa hali tegemezi.
Utapata sentensi kama vile: Kalamu hizo zingenunuliwa zingetumiwa darasani leo, imekanushwa kwa: Kalamu hizo sizingenunuliwa sizingetumiwa darasani leo.
Vilevile unaweza kukumbana na sentensi: Nguo hizo zingalichafuka zingalifuliwa na dobi, imekanushwa kwa: Nguo hizo sizingalichafuka sizingalifuliwa na dobi.
Sentensi hizo zimekanushwa visivyofaa.
Kiambishi cha ukanusho wa hali tegemezi ‘si’ kimetumiwa kabla ya kiambishi kitenzi cha wingi wa ngeli ya I-ZI.
Ili kuzisahihisha sentensi hizo tunafaa kusema: Kalamu hizo zisingenunuliwa sizingetumiwa darasani leo. Nguo hizo zisingalichafuliwa zisingalifuliwa na dobi.
Mwanafunzi mwenye changamoto ya kukanusha sentensi za hali tegemezi zilizotungwa kwa kutumia nomino za wingi ngeli ya I-ZI anafaa kufanya mazoezi ya kuandika sentensi za aina hiyo na kuzikanusha.