Habari Mseto

IPOA yamtuza mkuu wa kituo cha polisi kwa kupambana na uhalifu

Na FLORAH KOECH July 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Kabarnet, Kaunti ya Baringo, Shamza Abedi, alishtuka alipopokea taarifa kuwa maafisa wa Mamlaka Huru ya Kusimamia Utendakazi wa Polisi (IPOA) walikuwa wakimtafuta.

Kwa kuwa IPOA huchunguza malalamishi dhidi ya maafisa wa polisi, Bi Abedi alihofia huenda mmoja wa maafisa wake alihusishwa na utovu wa nidhamu au kulikuwa na malalamishi dhidi ya kituo chake.

“Lakini walipofika nilishangaa waliponipa tuzo badala ya kuanza uchunguzi,” alisema.

Katika tukio lisilo la kawaida, IPOA ilimtunuku afisa huyo kwa juhudi zake za kurejesha usalama katika mtaa maarufu wa Zombie Street, uliokuwa umejaa wauzaji wa dawa za kulevya, pombe haramu, makahaba na wahalifu.

Akimkabidhi tuzo hiyo katika Kituo cha Polisi cha Kabarnet, Kamishna wa IPOA Boniface Samati Kemboi alisema Bi Abedi amefanya kazi ya kipekee kwa kurejesha utulivu katika Kabarnet na maeneo yake.

“Leo hatujakuja kuchunguza afisa wa polisi bali kumpongeza kwa juhudi zake za kupambana na pombe haramu, dawa za kulevya na uhalifu. Tumeshuhudia mabadiliko makubwa yaliyotokana na kazi yake,” alisema Bw Kemboi.

Aliongeza kuwa ingawa IPOA inajulikana kwa kuwachunguza maafisa wanaokiuka sheria, pia ina wajibu wa kutambua na kuthamini wale wanaofanya kazi kwa uadilifu na kujituma.

Kabla ya operesheni hiyo, Zombie Street ilikuwa kitovu cha ulevi, matumizi ya dawa za kulevya, ukahaba na uporaji. Wakazi wengi waliogopa kupita katika eneo hilo mchana na usiku kutokana na visa vya uhalifu.

Baada ya kuhamishwa Kabarnet, Bi Abedi alianzisha doria za mchana na usiku kwa ushirikiano na wananchi kupitia mpango wa polisi jamii.

Polisi walivamia vilabu haramu vya pombe na kuvunja mtandao wa wasambazaji wa dawa za kulevya.

Kuanzia Novemba mwaka jana hadi Mei mwaka huu, zaidi ya washukiwa 10 wa biashara ya dawa za kulevya na watu zaidi ya 900 waliohusishwa ulevi na kufanya fujo walikamatwa na kufikishwa mahakamani.

Baadhi ya waliokamatwa ni wanawake waliokuwa wamebeba watoto migongoni huku wakidaiwa kujihusisha na shughuli haramu. Watoto hao waliokolewa na kupelekwa katika vituo vya malezi.

Wakazi wanasema operesheni hiyo imeleta mabadiliko makubwa. Biashara zimeimarika, visa vya uporaji vimepungua na familia zilizokuwa zimeathiriwa na uraibu zimeanza kuungana tena.

Mkazi mmoja, Caren Kipng’ok, alisema wananchi wamempa Bi Abedi jina la utani “Suluhu” kwa sababu ameleta suluhisho kwa matatizo yaliyokuwa yakikumba Kabarnet.

Akipokea tuzo hiyo, Bi Abedi alisema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano kati ya polisi na wananchi.

“Nawashukuru wananchi kwa kushirikiana nasi kupitia polisi jamii. Nilipohamishwa hapa sikujua kuwa kazi niliyokuwa nikifanya ingegusa maisha ya watu wengi kiasi hiki. Leo Kabarnet imerejea katika utulivu wake wa zamani na hata wake wa watu hunitania kwamba waume wao sasa hurudi nyumbani mapema badala ya kukesha Zombie Street,” alisema.