Habari

Majambazi sasa wanatumia wanawake kupora watu barabarani

Na ERIC MATARA NA PIUS MAUNDU July 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WANAWAKE wanatumiwa na magenge ya wahalifu kuwatega madereva kwenye barabara kuu nchini kabla ya kushambuliwa kwa bunduki na kuporwa magari, bidhaa na mali nyingine, uchunguzi umebaini.

Mbinu hiyo mpya imeibuka huku visa vya ujambazi wa kutumia silaha vikiongezeka katika barabara kuu za Nairobi-Mombasa, Nairobi-Nakuru-Eldoret na maeneo mengine muhimu ya uchukuzi.

Maafisa wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) wanasema wanawake wanaovutia hupelekwa kandokando ya barabara wakijifanya wamekwama, wamepata hitilafu ya gari au wanahitaji msaada wa dharura. Madereva wanaposimamisha magari yao kuwasaidia, majambazi wanaojificha huwavamia na kutekeleza uporaji.

Mpelelezi mmoja mkuu wa DCI alisema wanawake hao hutumiwa kama chambo ili kuwafanya madereva wapuuze tahadhari kabla ya wenzao kushambulia.

“Tumewakamata wanawake kadhaa wanaohusishwa na ujambazi huu. Wao hutumiwa kuwavutia madereva wa malori na magari mengine kabla ya washirika wao wenye silaha kuvamia walengwa,” alisema afisa huyo.

Katika mojawapo ya matukio yaliyotikisa mamlaka, mnamo Aprili 9 mwaka huu, lori lililokuwa likisafirisha bidhaa za thamani ya mamilioni ya pesa kutoka Nairobi kuelekea Mombasa lilitekwa nyara eneo la Ikanga kwenye Barabara Kuu ya Nairobi-Mombasa.

Ripoti ya polisi ilionyesha kuwa mwanamke mmoja alitokea ghafla kichakani kana kwamba alitaka kuvuka barabara. Dereva alipojaribu kumkwepa ili asimgonge, lori lilitoka barabarani na ndipo watu watano waliokuwa wamejificha wakaanza kumvamia.

Majambazi hao waliwafunga pingu dereva na msaidizi wake, kisha mmoja wao akaendesha lori kuelekea Mombasa. Waathiriwa walitupwa njiani huku wahalifu wakitoroka na lori pamoja na mzigo.

Baadaye wapelelezi waliwakamata washukiwa sita, akiwemo mwanamke mmoja, na kufanikiwa kupata nambari za usajili za lori hilo.

Wiki mbili zilizopita, daktari Reuben Osiemo pia alinusurika kutekwa nyara alipokuwa akisafiri kwenda Mombasa kuhudhuria warsha.

Alipofika karibu na Makindu, mwanamke aliyekuwa amevalia vizuri alimpa ishara ya kusimama kana kwamba alikuwa amekwama.

Daktari huyo alipunguza mwendo ili kuzungumza naye, wahalifu wawili walitokea kichakani na kujaribu kuteka gari lake aina ya Toyota Land Cruiser.

Kwa bahati nzuri, polisi waliokuwa wakishika doria walifika haraka na kufyatua risasi hewani, hatua iliyowalazimu majambazi kutorokea msituni.

Mbali na kutumia wanawake, polisi wanasema magenge hayo pia hujifanya maafisa wa polisi au wa Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru Kenya (KRA).

Huvaa jezi au koti ya kuakisi mwanga, hubeba redio za mawasiliano na kusimamisha magari kana kwamba wanafanya ukaguzi rasmi.

Katika visa vingine, huweka mawe au vizuizi barabarani ili kulazimisha madereva kupunguza mwendo kabla ya kushambuliwa.

Pia hurusha misumari barabarani ili kupasua magurudumu ya magari, hasa malori ya masafa marefu, kabla ya kuyateka.

Mkurugenzi wa DCI, Mohamed Amin, alisema idara hiyo imeunda kikosi maalumu kuwafuatilia wahalifu hao.

“Tumeendesha operesheni za kijasusi zilizowezesha kukamatwa kwa washukiwa wengi na kurejesha baadhi ya bidhaa zilizoibwa. Huu ni ujumbe kwamba sheria itawapata wote wanaowahangaisha wasafiri,” alisema Amin.

Aliongeza kuwa uchunguzi unatumia teknolojia ya kisasa, ikiwemo kufuatilia rekodi za simu na kubaini maeneo ya washukiwa kupitia mitandao ya mawasiliano.

Mnamo Juni 27 mwaka huu, maafisa wa DCI waliwakamata washukiwa wanane wanaodaiwa kuwa vinara wa mtandao wa ujambazi uliokuwa ukilenga magari ya kampuni za usafirishaji na malori yaliyobeba bidhaa za thamani ya mamilioni ya pesa.

Kwa mujibu wa Amin, genge hilo lilikuwa na mtandao mpana Nairobi na Kisumu na lilikuwa likijifanya maafisa wa DCI na KRA kabla ya kuelekeza magari kwenye maeneo ya faragha ambako mizigo ilihamishwa kwenye magari mengine na kutoweka.

Katika operesheni hiyo, polisi walipata vifaa vya mawasiliano na magari yanayoaminika kutumiwa kutekeleza uhalifu huo.

Wakati huo huo, polisi wameonya madereva kuwa waangalifu wanaposafiri, hasa usiku, na wasisimamishwe na watu wasiowafahamu katika maeneo yasiyo salama.