Gachagua na Murkomen wapondana kuhusu ghasia eneo la Ol Kalou
VITA vya kisiasa kati ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen vimechukua mkondo mpya baada ya wawili hao kurushiana lawama kuhusu ghasia zilizoshuhudiwa Ol Kalou, Kaunti ya Nyandarua.
Mzozo huo umeibua maswali kuhusu chanzo cha vurugu hizo huku kila upande ukimlaumu mwenzake, joto la siasa likizidi kupanda kuelekea uchaguzi mdogo wa Julai 16, 2026 na uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.
Kupitia ujumbe aliouchapisha katika mtandao wa X, Bw Gachagua alidai serikali ilitumia polisi na makundi ya wahuni kuvuruga shughuli za chama chake cha Democracy for the Citizens Party (DCP).
Alisema wafuasi wa chama hicho walikamatwa, kupigwa na kutishwa kabla ya kukimbilia Hoteli ya Royal Garden, ambako alidai walizingirwa na maafisa wa usalama pamoja na watu aliowataja kuwa wahuni waliotumwa na serikali.
“Timu zetu zimekwama katika Hoteli ya Royal Garden zikizingirwa na polisi pamoja na magenge wanaofadhiliwa na serikali. Wahuni kwa sasa wanavamia hoteli hiyo,” alidai Bw Gachagua.
Hata hivyo, Waziri Murkomen alikanusha madai hayo na kumshutumu Gachagua kwa kile alichokiita njama za kujionyesha kama mwathiriwa ili kupata huruma ya umma.
“Bw Rigathi Gachagua, tunazijua mbinu zako na juhudi zako za kutumia hila za kisiasa. Jaribu kuleta vurugu Ol Kalou, utaona kitakachotokea,” alisema Murkomen kupitia ukurasa wake wa X.
Waziri huyo aliendelea kumshutumu Gachagua kwa madai ya kuwachochea watu kushiriki katika vitendo vya fujo na kuwaonya Wakenya dhidi ya kujiingiza katika vitendo vya uvunjaji wa sheria.
“Yeyote anayechochewa na Bw Gachagua kushiriki katika vurugu ajiepushe nazo kwa sababu matokeo yake yatakuwa mabaya,” alionya Murkomen.
Hii si mara ya kwanza kwa Waziri huyo kumshambulia kisiasa Gachagua. Wiki iliyopita akiwa katika hafla Kaunti ya Elgeyo Marakwet, Murkomen alidai aliyekuwa Naibu Rais ndiye anayechochea ghasia nchini.
“Sababu inayomfanya Gachagua aniogope ni kwamba namfahamu vizuri. Najua yeye ndiye baba wa vurugu nchini Kenya,” alisema Murkomen.
Kwa upande wake, Gachagua ameendelea kusisitiza kuwa vyombo vya usalama vinatumiwa kukandamiza upinzani na kuwanyanyasa wafuasi wake.