Junior Starlets yaitandika Afrika Kusini, sasa guu moja ndani ya Kombe la Dunia U-17
TIMU ya taifa ya soka ya vichuna chini ya miaka 17, Junior Starlets, imesalia na dakika 90 pekee kufuzu kwa Kombe la Dunia la Mabinti kwa mara ya pili.
Warembo hao wanaonolewa na Mildred Cheche waliinyorosha wenyeji Afrika Kusini 2-0 katika mechi ya mkondo wa kwanza ya raundi ya mwisho ya kufuzu Kombe la Dunia la kwa wasichana chini ya miaka 17, iliyochezwa jioni jana katika Uwanja wa Lucas Moripe, Pretoria.
Beki Faith Boke aliipa Kenya uongozi dakika ya 14 kabla ya mshambuliaji Brenda Achieng’ kufunga bao la pili dakika ya 61 na kuwapa Starlets ushindi muhimu ugenini.
Mechi ya marudiano itachezwa Jumapili hii katika Uwanja wa Kitaifa wa Nyayo jijini Nairobi, kuanzia saa tisa alasiri.
Ushindi huo umeiweka Kenya katika nafasi nzuri ya kufuzu kwa fainali zitakazoandaliwa Morocco kati ya Oktoba 17 na Novemba 8.
Starlets wanahitaji sare ya aina yoyote au hata kupoteza kwa bao moja pekee nyumbani ili kukata tiketi ya Kombe la Dunia.
Kwa upande mwingine, Afrika Kusini, maarufu kama Bantwana, italazimika kushinda kwa tofauti ya mabao matatu au zaidi ili kufuzu.
Mshindi wa jumla ya mabao katika mechi ya marudiano, atajikatia tiketi ya mwisho ya Afrika kushiriki Kombe la Dunia.