Siasa za ubabe: Pesa itaongea katika uchaguzi wa 2027
IKIWA kuna jambo ambalo wachambuzi wa siasa wanakubaliana nalo, ni kwamba uchaguzi mkuu wa 2027 unatarajiwa kuwa wa gharama kubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa nchini.
Kuanzia matumizi ya helikopta za kukodi, wataalamu wa kampeni, mikakati ya kidijitali hadi kampuni za tafiti za maoni, siasa zimegeuka kuwa biashara inayohitaji mabilioni ya fedha. Hali hii imezua hofu kwamba demokrasia inageuka kuwa uwanja wa matajiri na wafadhili wao pekee.
Kutokana na hali hiyo, Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imependekeza kanuni mpya za kudhibiti matumizi ya fedha za kampeni ili kuongeza uwajibikaji na uwazi.
Chini ya mapendekezo hayo yaliyochapishwa Julai 6, 2026, mgombea urais ataruhusiwa kutumia hadi Sh4.44 bilioni katika kampeni, huku vyama vya kisiasa vinavyowasilisha wagombea kuanzia udiwani hadi urais vikipewa matumizi ya juu ya Sh17.7 bilioni.
Wagombeaji wa ugavana, useneta na uwakilishi wa wanawake watatumia kati ya Sh12.3 milioni na Sh123 milioni kulingana na ukubwa wa eneo lao, huku wagombeaji wa ubunge wakiruhusiwa kutumia kati ya Sh17.5 milioni na Sh123 milioni. Wagombea udiwani watatakiwa kutumia kiwango cha juu cha kati ya Sh2.5 milioni na Sh20 milioni.
Mwenyekiti wa IEBC Erastus Ethekon alisema kanuni hizo zinalenga kuhakikisha fedha za kampeni zinatumika kwa uwazi na uwajibikaji.
Hata hivyo, kabla ya kanuni hizo kuanza kutekelezwa, mjadala kuhusu matumizi ya fedha umechacha, hasa kufuatia kampeni za uchaguzi mdogo wa Ol Kalou.
Viongozi wa upinzani wakiongozwa na Rigathi Gachagua wameshutumu serikali kwa kutumia fedha nyingi na rasilimali za umma kushawishi wapigakura.
“Maafisa wa serikali Ol Kalou ni wengi kuliko wapigakura. Helikopta zimejaa angani kiasi cha karibu kugongana,” alisema Bw Gachagua.
Katika taarifa ya pamoja, David Maraga, Kalonzo Musyoka, Martha Karua, Fred Matiang’i na Edwin Sifuna walidai vitendo hivyo vinakiuka Sheria ya Makosa ya Uchaguzi, ikiwemo kutoa hongo kwa wapigakura na matumizi ya rasilimali za umma kisiasa. Lakini msemaji wa serikali Isaac Mwaura alitaja madai hayo kuwa ya kupotosha, huku Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Kimani Ichung’wah akidai ni ya uongo na propaganda.
Mbali na kampeni zinazoonekana hadharani, kuna mtandao mkubwa wa wafadhili ambao hufadhili wagombeaji kwa siri licha ya sheria kuwataka kujitokeza wazi.
Katika uchaguzi wa 2022, aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta aliwashawishi wafanyabiashara wa eneo la Mlima Kenya chini ya Mt Kenya Foundation kumuunga mkono Raila Odinga kupitia michango ya mabilioni ya fedha.
Kwa upande mwingine, viongozi wa muungano wa upinzani wanakiri kuwa kukabiliana na nguvu za kifedha za serikali iliyoko madarakani ni changamoto kubwa.
Profesa Karuti Kanyinga wa Chuo Kikuu cha Nairobi amewahi kukadiria kuwa kampeni za urais nchini hugharimu takriban Sh14 bilioni.
Hata hivyo, Martha Karua anasema uchaguzi haupaswi kuamuliwa na fedha bali uadilifu na uwezo wa mgombeaji.
Si mashindano ya fedha. Wakenya wanapaswa kuwachagua viongozi kwa tabia, rekodi na uwezo wao wa kuhudumia wananchi,” alisema.
Aliongeza kuwa chama chake hakitakopa wala kutumia rasilimali za umma kufadhili kampeni.
Nao Dkt Fred Matiang’i, Seneta Okong’o Omogeni na aliyekuwa Waziri Mithika Linturi wameeleza wasiwasi kuhusu matumizi makubwa ya fedha na helikopta katika chaguzi ndogo za hivi majuzi.
Mashirika ya kutetea demokrasia yameonya kuwa sheria za kufadhili kampeni tayari zipo lakini hazitekelezwi ipasavyo.
Mkurugenzi wa Centre for Multiparty Democracy (CMD), Frankline Mukwanja, amesema IEBC inapaswa kusimamia kikamilifu utoaji wa taarifa za michango na matumizi ya kampeni kwa wakati halisi pamoja na kuwaadhibu wanaokiuka sheria. Kwa upande wake, mratibu wa Elections Observation Group (ELOG), Mulle Musau, alisema Sheria ya Ufadhili wa Kampeni ya mwaka 2013 tayari inaeleza vyanzo vinavyoruhusiwa vya fedha na inawataka wagombeaji kufichua wafadhili wao.
Mchambuzi wa siasa Mark Bichachi anaamini upinzani utahitaji kutumia teknolojia zaidi kuliko fedha ili kushindana na serikali, huku Profesa Gitile Naituli akisisitiza kuwa ingawa fedha ni muhimu, hazitoshi kushinda uchaguzi.
Bila utekelezaji madhubuti wa sheria na uwazi kuhusu fedha za kampeni, wadau wanaonya kuwa uchaguzi wa 2027 unaweza kutawaliwa na nguvu ya fedha badala ya sera, uongozi na maslahi ya wananchi.