Makala

Hofu ya Koome kuhusu magenge ya wahuni yanayodhaminiwa na wanasiasa

Na BENSON MATHEKA July 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JAJI Mkuu Martha Koome ameonya kuhusu ongezeko la magenge ya uhalifu yanayodaiwa kufadhiliwa na wanasiasa, akisema hali hiyo inatishia usalama wa taifa huku idadi ya makundi hayo ikiendelea kuongezeka.

Akizungumza katika mahojiano  na kituo kimoja cha televisheni Jumapili, Koome alisema ripoti ya Kituo cha Utafiti wa Uhalifu (Crime Research Centre) inaonyesha kuwa kuna zaidi ya magenge 600 ya uhalifu yanayofanya kazi kote nchini, na huenda sasa idadi hiyo imefikia karibu 1,000.

Kwa mujibu wa Jaji Mkuu, baadhi ya wanasiasa huunda na kufadhili makundi hayo ili kutekeleza ajenda zao za kisiasa.

“Ripoti tuliyopokea kutoka Kituo cha Utafiti wa Uhalifu inaonyesha kuwa kila mara kuna magenge mapya yanayoanzishwa na wanasiasa. Wanapoenda kwenye mikutano ya kisiasa huandamana na makundi hayo ambayo hushangilia viongozi wao, kuwazomea wapinzani na wakati mwingine kushiriki vitendo vya vurugu,” alisema Koome.

Aliongeza kuwa ongezeko la magenge hayo linazua wasiwasi mkubwa kuhusu usalama wa nchi na utekelezaji wa sheria.

“Ripoti hiyo ilionyesha kulikuwa na zaidi ya magenge 600 nchini. Yanaendelea kuongezeka kila siku, na naamini sasa huenda yamefikia karibu 1,000. Hili linatia wasiwasi mkubwa,” alisema.

Koome alisema idadi kubwa ya magenge hayo imefanya iwe vigumu kwa maafisa wa usalama kukusanya ushahidi wa kutosha ili kuwafikisha wahusika mahakamani. Hata hivyo, aliwataka polisi kutumia zaidi taarifa za kijasusi na hatua za kuzuia uhalifu kabla ya kutokea.

“Polisi wanawafahamu watu hawa, na wanaweza kuzuiwa hata kabla hawajatenda uhalifu,” alisema.

Kauli za Jaji Mkuu zinajiri siku chache baada ya kiongozi wa People’s Liberation Party (PLP), Martha Karua, kutoa wito wa mazungumzo ili kukabiliana na ongezeko la makundi ya wahuni yanayotumiwa katika siasa.

Akizungumza katika ibada ya kanisa huko Ahero, Karua aliwataka Wakenya kukataa matumizi ya vurugu katika kutatua tofauti za kisiasa, akisema wanaojihusisha na vitendo hivyo ni wanajamii wanaoweza kushawishiwa kupitia mazungumzo.

“Tukatae kutumia vurugu kutatua tofauti zetu. Wahuni hawa wanatoka katika familia na jamii zetu. Tuzungumze na wenzetu ili kupata suluhu ya kudumu,” alisema.

Kauli za viongozi hao zinajiri kukiwa na wasiwasi unaoongezeka kuhusu visa vya vurugu katika mikutano ya kisiasa na maandalizi ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.