Murkomen atetea polisi kuhusu uhuni: ‘Kenya iko salama kuliko wakati mwingine wowote ule’
WAZIRI wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen, ametetea uongozi wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi huku maswali yakiendelea kuibuka kuhusu kuenea kwa ghasia katika uchaguzi mdogo eneo bunge la Ol Kalou wiki iliyopita.
Kauli yake inajiri licha ya kuagiza uchunguzi baada ya uchaguzi huo uliogubikwa na vurugu, ambapo watu waliokuwa wamejifunika nyuso walidaiwa kuwashambulia wakazi na hata kuwafyatulia risasi maafisa wa polisi waliokuwa kazini.
Akizungumza Alhamisi wakati wa uzinduzi wa Mfumo wa Kisasa wa Kutambua Alama (MBIS) katika makao makuu ya Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), Bw Murkomen alisema ana imani kamili na uongozi wa Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja na kuwataka maafisa wa DCI kukabiliana vikali na magenge ya wahalifu.
“Heshima yangu kwa Inspekta Jenerali ni kubwa. Nina imani kamili na uongozi wake. Aliteuliwa na Rais, akathibitishwa na Bunge na tangu ashike wadhifa huo ametekeleza majukumu yake kwa heshima na utaalamu,” alisema.
Hata hivyo, hakueleza kwa nini hadi sasa hakuna mshukiwa aliyekamatwa au kufikishwa mahakamani, wiki moja baada ya watu wenye silaha kuzua hofu Ol Kalou, kuwaua watu wawili na kuvuruga uchaguzi huo.
Tukio hilo lilirekodiwa kwa picha na video zilizokuwa zikisambazwa mitandaoni, huku nambari za usajili za baadhi ya magari yaliyodaiwa kutumiwa na washambuliaji pia zikichapishwa.
Bw Murkomen alisisitiza kuwa hali ya usalama nchini imeimarika kwa kiasi kikubwa.
“Kenya iko salama kuliko wakati mwingine wowote. Mashambulizi, ujambazi, ugaidi, wizi na uhalifu vimepungua. Takwimu zinajieleza zenyewe,” alisema.
Kauli hiyo imeibua mjadala huku serikali ikikosolewa kwa kujivuta kuhusu uchunguzi wa ghasia za Ol Kalou ambapo magenge yalishambulia wananchi, wanahabari na wafuasi wa wanasiasa hadharani.
Ingawa mapema wiki hii Rais William Ruto aliagiza maafisa wa usalama kuwakamata wahalifu na kukomesha magenge ya wahuni, hakuna washukiwa wa ghasia hizo waliotangazwa kukamatwa rasmi.
Badala yake, Bw Murkomen aliwahakikishia maafisa wa DCI kuwa serikali inaunga mkono juhudi zao za kupambana na wahalifu.
“DCI, tunawaunga mkono. Shughulikieni wahalifu hawa bila kuyumba. Sasa mna teknolojia ya kisasa ya kuwatambua,” alisema.