ODM sasa yaelekeza shoka kwa Osotsi Seneti baada ya ‘kummaliza’ Sifuna
CHAMA cha ODM sasa kinapanga kumng’oa Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi katika wadhifa wa mwenyekiti wa Kamati ya Uwekezaji wa Kaunti na Hazina Maalum ya Seneti (CPIC), wiki moja tu baada ya Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kuondolewa kama Naibu Kiongozi wa Wachache katika Seneti.
Taarifa zinaonyesha kuwa maseneta walioteuliwa wanaohudumu katika kamati hiyo wanashinikizwa na viongozi wa ODM pamoja na chama tawala cha UDA kutia saini hoja ya kutokuwa na imani na uongozi wa Bw Osotsi ili kuharakisha kuondolewa kwake.
Vyanzo ndani ya ODM vimesema chama hicho kinapanga kumweka Seneta wa Taita Taveta Johnes Mwaruma katika nafasi yake.
Kamati hiyo ilipanga kufanya kikao jana jioni kujadili mabadiliko hayo, lakini kikao hicho hakikuwa kimefanyika kufikia wakati wa kuchapishwa kwa taarifa hii.
Kamati ya CPIC inaongozwa na Bw Osotsi huku Seneta wa Migori Eddy Oketch akiwa makamu mwenyekiti.
Wanachama wengine ni Peris Tobiko, Raphael Chimera, George Mbugua, William Kisang, Agnes Muthama, Beth Syengo na Hamida Kibwana.
Bw Osotsi alithibitisha kufahamu mpango huo lakini akasema ni “wa kisiasa” unaolenga viongozi wa mrengo wa Linda Mwananchi, unaompinga Rais William Ruto.
“Huu ni hila ya kisiasa inayoratibiwa na Oburu Oginga pamoja na Rais Ruto. Kamati hii imefanya kazi kubwa kwa zaidi ya miaka mitatu na nusu. Hakuna msingi wa kuniondoa kwa madai ya utendakazi duni,” alisema.
Alisema kamati hiyo imechangia kuboresha usimamizi wa fedha za kaunti na kampuni za maji nchini na kwamba mpango wa kumng’oa unafanana na ule uliomuondoa kama naibu mwenyekiti wa ODM.
Bw Osotsi ni miongoni mwa viongozi wa mrengo wa Linda Mwananchi unaojumuisha Seneta Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, ambao wanapinga azma ya Rais Ruto kutafuta muhula wa pili mwaka wa 2027.
Katika miezi ya hivi majuzi, mrengo wa Kiongozi wa ODM Oburu Oginga umekuwa ikiwashinikiza viongozi hao kuondolewa katika nyadhifa mbalimbali za chama na Bunge.
Mnamo Machi 27, 2026, Bw Osotsi aliondolewa kama mmoja wa manaibu viongozi wa ODM wakati wa Mkutano Maalum wa Wajumbe wa Kitaifa.