Waziri Duale motoni kwa kauli tata ya kueneza ukabila
WAZIRI wa Afya, Aden Duale analaumiwa kufuatia matamshi yake kuhusu jamii za Kenya kuzua mjadala mkubwa nchini, huku Tume ya Kitaifa ya Uwiano na Utangamano (NCIC) ikianzisha uchunguzi kubaini iwapo kauli hizo zilichochea mgawanyiko wa kikabila.
Video iliyosambaa kwa kasi mitandaoni ilimuonyesha Bw Duale akizungumza kwa lugha ya Kisomali katika mkutano uliofanyika eneo la Lafey, Kaunti ya Mandera, Julai 20, 2026.
Katika hotuba hiyo, alisema utawala wa Rais William Ruto umefanya maendeleo makubwa zaidi katika eneo la Kaskazini Mashariki kuliko tawala za marais waliotangulia, akiwemo Hayati Jomo Kenyatta, Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta.
Pia alieleza kuwa jamii ya Wasomali ina watu takriban milioni 41 duniani na kudai kuwa kwa muda mrefu baadhi ya jamii zimekuwa zikitawala siasa na nafasi muhimu serikalini huku maeneo mengine yakisalia nyuma.
Hata hivyo, matamshi hayo yamekosolewa vikali na viongozi wa kisiasa na wananchi walioyataja kuwa ya uchochezi na yanayoweza kuvuruga mshikamano wa kitaifa.
Mnamo Ijumaa, NCIC ilisema imeanza uchunguzi kuhusu matamshi hayo.
“Timu ya uchunguzi ya Tume inaendelea kufanya uchunguzi bila upendeleo kuhusu matamshi hayo. Tunawahimiza viongozi kujiepusha na kauli zinazoweza kuchochea chuki za kikabila na kuwakumbusha kuwa Kenya ni ya Wakenya wote,” alisema mwenyekiti wa NCIC, Askofu Kepha Omae.
Aliongeza kuwa tume itaendelea kuchukua hatua madhubuti dhidi ya mtu yeyote atakayehatarisha umoja wa taifa, hasa wakati nchi inaelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.
Gavana wa Kirinyaga, Anne Waiguru alisema kauli za Duale zilikuwa za kusikitisha na hatari.
“Ni jambo hatari na la kupotosha kueleza changamoto za kisiasa kwa misingi ya ukabila. Kauli kama hizo hazikubaliki kutoka kwa kiongozi mwenye hadhi ya Waziri wa Baraza la Mawaziri,” alisema.
Suala hilo pia liliibuliwa katika Seneti ambapo Maseneta Enoch Wambua (Kitui), Ledama Ole Kina (Narok) na Abdul Haji (Garissa) walitaka viongozi kuwa waangalifu wanapozungumza kuhusu masuala ya kikabila.
Seneta Ole Kina alisema viongozi wana jukumu la kuwaunganisha Wakenya.
“Nilimsikia Waziri akilinganisha jamii na kuacha taswira kwamba jamii moja ni bora kuliko nyingine. Kauli kama hizi zinaweza kurudisha taifa kwenye siasa za migawanyiko,” alisema.
Seneta Wambua alionya kuwa matamshi hayo yanawakumbusha Wakenya hali ilivyokuwa kabla ya uchaguzi wa mwaka 2007.
“Tuliona kilichotokea mwaka 2007 baada ya viongozi kuanza kutumia lugha ya chuki. Tunapoelekea uchaguzi wa 2027, viongozi wanapaswa kuhubiri amani badala ya kuwagawa wananchi,” alisema.
Seneta Abdul Haji alisema iwapo Duale alitoa matamshi hayo kama yalivyosikika kwenye video, basi ilikuwa makosa.
Aliyekuwa Mbunge wa Mukurweini Kabando wa Kabando pia alimkosoa Duale, akidai kauli zake zinaakisi msimamo wa utawala wa sasa.
Akijibu lawama hizo, Duale alisema kauli zake zilitokana na methali ya jadi ya Kisomali ambayo imetafsiriwa vibaya na kutumiwa kisiasa.
Alisema methali hiyo inamrejelea mnyama mwenye tabia ya kujinufaisha na inalenga watu au makundi yaliyozoea kunufaika na mamlaka na rasilimali kiasi kwamba inakuwa ugumu kukubali kugawa nafasi kwa jamii nyingine.
Kwa mujibu wa Duale, alichomaanisha ni kwamba tangu uhuru, eneo la Mlima Kenya limekuwa likishikilia nafasi za juu serikalini, ikiwemo urais au makamu wa rais, na kwamba Rais Ruto amejaribu kupanua ushirikishaji kwa kuwapa nafasi Wakenya kutoka jamii mbalimbali.
Pia alimshutumu aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kwa madai ya kutoa matamshi yaliyolenga Wasomali, ikiwemo kuita Kaskazini Mashariki eneo la ugaidi, kupinga kuondolewa kwa mfumo wa ukaguzi wa vitambulisho kwa Wasomali na kuhoji uteuzi wa Wasomali katika nyadhifa za serikali.
Alipoulizwa iwapo angeomba msamaha, Duale alisema taarifa aliyotoa tayari ilifafanua alichomaanisha.
“Maneno yangu yanajieleza yenyewe,” alisema.