Habari za Kitaifa

Hivi ndivyo msanii wa Bongo Matonya aliponyoka kesi ya ubakaji na mwanamke Mkenya

Na BRIAN OCHARO August 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MSANII wa Bongo Flava kutoka Tanzania, Sefu Ramadan almaarufu Matonya, aliponyoka kesi ya ubakaji iliyokuwa ikimuandama kufuatia ombi lililotolewa na mamake kwa mwanamke aliyekuwa amemshtaki.

Jambo hilo lilifanya Mahakama ya Shanzu, Mombasa kumuondolea kesi hiyo.

Imebainika kuwa mamake Matonya alimtafuta mfanyabiashara huyo wa Kenya na kumsihi amsamehe mwanawe.

Mwanamke huyo baadaye aliambia mahakama kuwa aliamua kuondoa kesi hiyo baada ya ombi la mama huyo pamoja na msongo wa mawazo alioupata kutokana na mchakato mzima wa kesi.

“Nimeamua kumsamehe mtuhumiwa kwa sababu kesi imeniletea msongo wa mawazo. Mamake mshukiwa ambaye ni mgonjwa alinifikia na kuniomba nimsamehe mwanawe,” alisema mwanamke huyo katika Mahakama ya Shanzu.

Stakabadhi za Mahakama zinaonyesha kuwa ombi hilo halikupingwa na upande wa mashtaka ambao uliiambia mahakama kuwa ulikuwa na maagizo ya kuondoa kesi hiyo.

“Kwa kuwa ombi la kuondoa mashtaka limeungwa mkono na upande wa mashtaka, kesi hii imeondolewa. Mtuhumiwa yuko huru,” iliamua mahakama, na kuamuru pia pasipoti ya Matonya irejeshwe, ilani iliyowekwa iondolewe na mdhamini wake kuachiliwa.

Kwa upande wake, Matonya, alitoa shukrani tu.

“Nashukuru. Naomba pasipoti yangu irejeshwe,” alisemaKatika kiapo chake, mlalamishi huyo alisisitiza kuwa uamuzi wake ulikuwa wa hiari bila kulazimishwa, kutishwa, kushawishiwa au kuahidiwa chochote.

“Ni uamuzi wangu binafsi kufuta kesi na najua nikishaifuta siwezi kuirudisha tena,” alisema.

Alieleza mahakama kuwa amepatana na mtuhumiwa na kuchagua kumsamehe.

Pia alitaja majukumu ya safari za mara kwa mara ambayo yangemzuia kuendelea kufika mahakamani.

Mwanamke huyo aliongeza kuwa kesi hiyo imemsababishia msongo wa mawazo, kuathiri maisha yake binafsi na mahusiano ya kijamii, na kumweka katika hali ya aibu na unyanyapaa wa kijamii.

“Kwa kuzingatia yote haya, sitaki tena kushiriki katika kesi hii. Ningependa kuendelea na maisha yangu na kuzingatia mambo yangu binafsi na majukumu ya baadaye,” alisema.

Aliongeza kuwa uamuzi wake ulitokana na maridhiano na mtuhumiwa, majukumu ya safari na athari za kihisia na kijamii za kesi, akisisitiza kuwa hakukuwa na masharti yoyote na ulikuwa ni tendo la msamaha pekee.

Rekodi za mahakama zinaonyesha kuwa Matonya alikana mashtaka Aprili 9, na kesi ikapangwa kusikizwa.

Jaribio la kwanza la kuondoa kesi lilifanyika Juni 11, lakini mahakama ilimtaka mlalamishi kuwasilisha kiapo cha kina kwa kuwa kesi ilihusisha tuhuma za ubakaji na ilikuwa ya maslahi ya umma.

Baada ya kiapo kuwasilishwa, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma ilipeleka faili kwa maafisa wa ngazi ya juu kwa idhini.

Julai 1, upande wa mashtaka ulithibitisha kuwa umepata idhini na ukaomba rasmi kuondoa mashtaka.

Mlalamishi aliapishwa, akathibitisha yaliyomo kwenye kiapo chake na kurudia sababu zake kabla ya mahakama kuruhusu ombi hilo, na hivyo kumaliza rasmi kesi ya jinai dhidi ya mwanamuziki huyo wa Tanzania.

Aprili 9, Matonya alishtakiwa kwa kosa la ubakaji na alikana mashtaka mawili ya unyanyasaji wa kijinsia.

Msanii huyo alishtakiwa kwa kosa kinyume na Kifungu cha 3(1)(a) kinachosomwa pamoja na Kifungu cha 3(3) cha Sheria ya Makosa ya Kingono.

Upande wa mashtaka ulidai kuwa Aprili 7, 2026, katika nyumba ya kifahari eneo la Nyali, Mombasa, mtuhumiwa alimbaka mlalamishi J.G. kwa kutumia nguvu.

Alikabiliwa pia na shtaka mbadala la kutenda kitendo kisicho cha heshima kwa mtu mzima, ambapo mahakama iliambiwa kuwa mtuhumiwa alimgusa sehemu za siri za mwanamke huyo bila ridhaa yake.