Habari Mseto

Ruto ataka walinzi wa kibinafsi na polisi kushirikiana katika ujasusi

Na KEVIN CHERUIYOT August 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

RAIS William Ruto ametangaza kuwa serikali itaanza kutumia taarifa za kijasusi zinazokusanywa na walinzi wa kampuni za kibinafsi ili kuimarisha vita dhidi ya uhalifu na kuimarisha usalama nchini.

Akizungumza Alhamisi katika Ikulu ya Nairobi alipokutana na mamia ya walinzi hao, Rais alisema mchango wao katika kulinda mali na maisha ya Wakenya ni muhimu na unapaswa kuunganishwa na juhudi za idara za usalama za serikali.

Aliagiza Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja, Mamlaka ya Kudhibiti Kampuni za Kibinafsi za Ulinzi (PSRA) na Afisi ya Rais kuandaa mfumo wa ushirikiano kati ya polisi na walinzi hao.

‘Mnafanya kazi muhimu ya kuhakikisha usalama. Pia mnakusanya taarifa nyingi kuhusu wahalifu. Ushirikiano huu utasaidia kuimarisha usalama nchini,’ alisema Rais Ruto.

Rais pia alisema sheria na kanuni zinazosimamia sekta hiyo zitarekebishwa ili kutoa nafasi ya kupandishwa vyeo kwa wanaofanya kazi kwa ufanisi.

Aidha, aliagiza taasisi za mafunzo ya walinda usalama kuoanisha mitaala yao ili kuwe na mfumo mmoja wa maendeleo ya taaluma.

Kuhusu mishahara, Dkt Ruto alisisitiza kuwa agizo la serikali la kuongeza kiwango cha chini cha mshahara kwa asilimia 15 bado linafaa kutekelezwa.

Alionya kampuni zinazowalipa walinzi chini ya kiwango cha chini cha mshahara, akisema baadhi hulipa wafanyakazi wao kiasi cha Sh6,000 pekee kwa mwezi.

Pia alizitaka kampuni zote kuhakikisha wafanyakazi wao wamejiandikisha kikamilifu katika Mamlaka ya Afya ya Kijamii (SHA).

Katika hotuba yake, Rais pia alitetea rekodi ya serikali yake na kusema wapinzani wake hawana ajenda ya maendeleo isipokuwa kampeni ya kutaka ahudumu muhula mmoja.