BAADA ya kufanya mikutano iliyofanikiwa katika kaunti za Bungoma na Trans Nzoia wiki mbili zilizopita, viongozi wa vuguvugu la Linda Mwananchi sasa wamehamishia kampeni zao katika ngome za kisiasa za aliyekuwa kinara wa ODM, Raila Odinga, wakilenga kuimarisha ushawishi wao huku wakipanua mtandao wao nchini.

Vuguvugu hilo linaloongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, linatarajia kufanya mikutano Busia Ijumaa kabla ya kuelekea Kakamega Jumamosi na Jumapili.

Viongozi hao wananuia kuvutia wafuasi wa ODM katika eneo la Magharibi huku chama hicho kikijitahidi kulinda ngome zake za jadi.

Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya, ambaye ameahidi kuunga mkono azma ya Bw Sifuna ya kuwania urais mwaka 2027, anatarajiwa kuwa mstari wa mbele katika juhudi za kuunganisha kura za jamii ya Mulembe kabla ya kampeni hizo kusambazwa kote nchini.

Ziara ya Kakamega pia inalenga ngome ya viongozi wanaounga mkono Rais William Ruto akiwemo Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya, Gavana Fernandes Barasa, Naibu Gavana Ayub Savula pamoja na zaidi ya wabunge wanane wanaounga mkono serikali jumuishi.

Ziara hiyo inafanyika wiki chache baada ya Bw Oparanya kufanya mkutano Malava ambapo alipendekezwa kuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto na kuahidi kuongoza juhudi za kuunganisha eneo la Magharibi kumuunga mkono Rais huku akiimarisha ODM.

Mnamo Agosti 16, msafara wa Linda Mwananchi utaelekea Homa Bay, mojawapo ya ngome kuu za ODM, ukiongozwa na Gavana Orengo.

Hii itakuwa mara ya pili kwa kundi hilo kuingia eneo la Luo Nyanza baada ya kufanya mkutano Kisumu.

Bw Orengo pia analenga kuimarisha nafasi yake kama msemaji wa kisiasa wa jamii ya Waluo kupitia mikutano Homa Bay, Kisumu na Siaya, huku mipango ikisukwa kupeleka kampeni hizo Migori.

Hata hivyo, maandalizi ya mkutano wa Homa Bay yamekumbwa na misukosuko baada ya kuripotiwa visa vya vurugu.

Mratibu wa muda wa Linda Mwananchi katika eneo hilo, Samuel Nyauke, alishambuliwa na kundi la vijana waliomshutumu kwa kupuuza uongozi wa kisiasa wa eneo hilo. Mali iliharibiwa baada ya mawe kurushwa katika ofisi yake, huku vijana sita wakikamatwa na baadaye kuachiliwa.

‘Kwa wanaotumia vurugu kulinda maeneo yao ya kisiasa, Kenya ni ya Wakenya wote. Hakuna vitisho vitakavyotuzuia. Tutakuwa Homa Bay kama ilivyopangwa,’ alisema Bw Orengo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Taifa wa ODM ambaye pia ni Gavana wa Homa Bay, Gladys Wanga, aliwataka wakazi kudumisha amani na kuruhusu kila chama kufanya siasa kwa uhuru.

‘ODM ilipigania uhuru wa kila Mkenya. Kila mtu ana haki ya kufika sehemu yoyote ya nchi na kuuza sera zake. Wanaotaka kuja Homa Bay wanakaribishwa,’ alisema Bi Wanga.

Aliwahimiza vijana kutoruhusu kutumiwa kuzua vurugu za kisiasa, akisisitiza kuwa tofauti za kisiasa hazipaswi kuvuruga amani.

Bi Wanga alisisitiza kuwa Homa Bay bado ni ngome ya ODM, huku akifichua kuwa chama hicho kina mpango wa kuongeza wanachama wake na kuimarisha mtandao wake kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.

Pia alithibitisha kuwa ODM itaendelea kushirikiana na serikali jumuishi na iko tayari kuanza mazungumzo na UDA kuhusu ushirikiano wa kisiasa kabla ya uchaguzi ujao.

‘ODM inaamini katika ushirikishaji wa wote na kuheshimiana kati ya jamii mbalimbali. Tuko tayari kwa uchaguzi wa 2027 na hatuna hofu ya kukabiliana na yeyote,’ alisema.