ODM yazua dhoruba kwa kung’ang’ania kiti cha Kindiki mkutanoni Naivasha
MVUTANO kuhusu nani atakuwa Naibu Rais iwapo Rais William Ruto atashinda muhula wa pili uliibuka katika kikao cha faragha cha viongozi wa Kenya Kwanza na ODM mjini Naivasha Jumatatu.
ODM ilisisitiza kuwa inataka nafasi hiyo katika makubaliano ya kisiasa yanayosukwa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Kwa mujibu wa duru kadhaa zilizohudhuria kikao hicho, Naibu Kiongozi wa ODM ambaye pia ni Gavana wa Kisii, Simba Arati, ndiye aliyeibua suala hilo.
Bw Arati alitaka serikali igawanye nafasi za serikali nusu kwa nusu, akisema nafasi ya Naibu Rais inapaswa kwenda kwa ODM kwa kuwa Rais Ruto, ambaye atakuwa mgombeaji urais wa muungano huo, anatoka UDA.
Kauli hiyo iliwakera baadhi ya wabunge wa Mlima Kenya, ambao walihisi kuwa madai hayo hayakuwa na heshima kwa Naibu Rais Kithure Kindiki, aliyekuwa ameketi karibu na Rais Ruto.
Hata hivyo, Mbunge wa Khwisero, Bw Christopher Aseka, alimtetea Bw Arati, akisema ODM inapaswa kuchukuliwa kama mshirika sawa na Kenya Kwanza na kupewa nafasi ya kumpendekeza mgombea mwenza.
“Hakuna mtu aliyetoka kwenye mkutano. Kulikuwa na manung’uniko na kutoridhika kutoka upande mwingine, jambo ambalo ni la kawaida kwa sababu suala hili limewahi kusababisha kutokubaliana,” alisema Bw Aseka.
Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa, Junet Mohamed, alithibitisha kuwa Bw Arati ndiye aliyeibua suala hilo, lakini akakanusha kuwa kulikuwa na mvutano.
“Ni kweli Arati aliliibua, lakini hakukuwa na ugomvi. Kwanza tulikubaliana kuunda muungano, kisha suala la nafasi litajadiliwa baadaye,” alisema Bw Mohamed.
Gavana wa Mombasa, Abdulswamad Nassir, alisema suala la Naibu Rais halikujadiliwa kwa kina katika mkutano huo.
“Hatukufikia kiwango hicho. Nafasi ya Naibu Rais itajadiliwa sambamba na kuundwa kwa muungano. Mazungumzo kama hayo hayawezi kufanywa katika chumba chenye viongozi zaidi ya 300,” alisema.
Kwa mujibu wa Bw Nassir, mkutano ulijikita zaidi katika mafanikio ya serikali katika kilimo, afya, uchumi na sekta nyingine ambazo viongozi waliambiwa wanapaswa kuelezea zaidi kuelekea uchaguzi wa 2027.
Hata hivyo, huku mvutano kuhusu nafasi hiyo ukiendelea, Prof Kindiki alikaa kwa utulivu kabla Rais Ruto kumwita kutoa muhtasari wa yaliyojadiliwa.
“Tunahitaji kufunga mjadala kuhusu tuliyojadili leo, na hakuna mtu bora anayeweza kuunganisha masuala ya uchumi, jamii, elimu, ugatuzi na diplomasia kuliko naibu wangu,” Rais Ruto alisema.
Kauli hiyo ilipokelewa kwa shangwe na wabunge wanaomuunga mkono Rais na ilitafsiriwa kama ishara ya imani ya Rais kwa Prof Kindiki.
Kwa dakika arobaini na tano, Prof Kindiki alielezea mafanikio ya serikali katika elimu, miundombinu, diplomasia na afya, bila kuingia katika mjadala kuhusu nafasi yake.
ODM imekuwa ikiongeza presha kutaka nafasi hiyo, huku Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya, akiwa mmoja wa viongozi wanaopendekezwa na chama hicho.
Bw Oparanya pia anapendekezwa na baadhi ya viongozi wa Magharibi mwa Kenya kama njia ya kukabiliana na umaarufu unaoongezeka wa Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna.
Hata hivyo, kura za maoni zinaonyesha Prof Kindiki bado anaongoza katika orodha ya wanaopendwa kuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto.
Kura ya maoni iliyotolewa Julai 13 ilimweka Prof Kindiki mbele kwa asilimia 34, akifuatiwa na Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga kwa asilimia 11, Kiongozi wa ODM Dr Oburu Oginga kwa asilimia tano na Waziri wa Madini Hassan Joho kwa asilimia nne.
Bw Oparanya, Spika wa Bunge Moses Wetang’ula na Waziri Mkuu Musalia Mudavadi pia wametajwa kama wanaoweza kuchukua nafasi hiyo.
Wakati huo huo, kamati ya watu 10 iliyoteuliwa kuandaa mpango wa pamoja wa uchaguzi wa 2027 imepewa mwezi mmoja kukamilisha kazi yake.
Kamati hiyo inatarajiwa kuandaa manifesto ya pamoja na makubaliano ya muungano kabla ya kuyawasilisha kwa Wakenya.
Duru zilizohudhuria mkutano huo zilisema ingawa pande hizo mbili zimekubaliana Rais Ruto ndiye atakuwa mgombea wa urais, suala linalobaki kuwa gumu ni nani atakuwa mwaniaji mwenza.
Kwa mujibu wa duru hiyo, uamuzi wa mwisho kuhusu mgombea mwenza utaachiwa Rais Ruto, ambaye atazingatia uwezo wa mgombea huyo kuleta kura kwa muungano.
“Huu ni mchezo wa nambari na kwa sasa mtu yeyote kutoka katika muungano anaweza kuchaguliwa. Iwe ni kutoka ODM au Kenya Kwanza, mgombeaji atachaguliwa kulingana na kura anazoweza kuleta,” duru iliongeza.
Hali hiyo inaashiria kuwa vita vya kumrithi Prof Kindiki kama Naibu Rais au kumdumisha vitakuwa miongoni mwa masuala makuu yatakayoamua muungano wa kisiasa kuelekea 2027.
TAARIFA YA CECIL ODONGO, SAMWEL OWINO, VITALIS KIMUTAI NA JOSEPH OPENDA