Teknolojia ya kidijitali inayolenga kuzuia migomo, ghasia shuleni
MIEZI michache iliyopita, tulishuhudia migomo, utovu wa nidhamu na mikasa ya moto shuleni.
Kampuni za teknolojia ya elimu zinaibua suluhisho za kidijitali zinazoweza kusaidia walimu kugundua mapema ikiwa wanafunzi hawaridhishwi na uongozi au kuna tatizo kabla mambo kuwa mbaya.
Mojawapo ya suluhisho hizo ni mfumo wa kutoa maoni kwa njia ya kidijitali uliobuniwa na kampuni ya teknolojia ya Kenya, Robisearch.
Mfumo huo huwawezesha wanafunzi kuripoti kwa siri masuala kama vile kuteswa, matumizi ya dawa za kulevya, unyanyasaji wa kingono na vitisho bila kufichua utambulisho wao.
Mkurugenzi Mkuu wa Robisearch, Robert Manyala, anasema changamoto nyingi shuleni huanza kama matatizo madogo ambayo uongozi hushindwa kuyagundua kwa wakati.
“Mtindo tunaouona kabla ya mzozo shuleni ni uleule: wanafunzi wanajua kuna jambo lisilo sawa kabla ya uongozi kufahamu, lakini hakuna njia salama ya kufikisha taarifa hiyo kwa walio mamlakani,” alisema.
Anaongeza kuwa mfumo huo unalenga kuziba pengo hilo kwa kuwapa wanafunzi nafasi ya kuripoti matatizo yanapoanza badala ya kusubiri hadi yaibuke na kuwa mkasa, mgomo au ghasia.
Kwa miaka mingi, shule nchini zimekuwa zikikumbwa na visa vya wanafunzi kuteketeza mabweni na madarasa, migomo na vurugu.
Baadhi ya wataalamu wa elimu wamehusisha visa hivyo na mawasiliano duni kati ya wanafunzi na wasimamizi wa shule.
Wanafunzi wanaweza kuogopa ‘kukujiwa’ wanaporipoti matatizo kupitia njia za kawaida.
Manyala anasema hata visanduku vya mapendekezo vya kawaida na mfumo wa viranja vinaweza kuwa na mapungufu.
Kupitia mfumo huo wa kidijitali, mwanafunzi anaweza kuwasilisha malalamiko kwa kutumia simu au kifaa cha shule bila kuandika jina, nambari ya simu au taarifa nyingine inayoweza kumtambulisha.
Taarifa hizo hupelekwa kwenye dashibodi salama inayoweza kufikiwa na maafisa walioidhinishwa pekee.
Malalamiko kuhusu uonevu, unyanyasaji wa kingono, vitisho, matumizi ya dawa za kulevya na masuala mengine hatari huainishwa kama ya dharura ili hatua zichukuliwe haraka.
Kila malalamiko huwekewa muda na kurekodiwa kidijitali, hatua ambayo Manyala anasema inasaidia kuhakikisha taarifa muhimu hazipotei au kupuuzwa.
Mfumo huo pia huwawezesha wakuu wa shule kufuatilia malalamiko kwa wakati halisi kupitia mtandao hata wanapokuwa nje ya shule.
Hata hivyo, Manyala anasisitiza kuwa teknolojia si suluhisho la matatizo yote yanayowakabili wanafunzi.
“Huu haufai kutumika kama mbadala wa washauri, Ni chombo cha kutoa tahadhari mapema ili kuhakikisha wanaohusika wanapata taarifa kabla tatizo halijawa kubwa,” alisema.