Sifuna: Tulinasa simu ya polisi mmoja aliyeshirikiana na wahuni, tutaitumia kama ushahidi
KINARA wa vuguvugu la kisiasa la Linda Mwananchi Edwin Sifuna amesema wanayo katika hifadhi yao chombo cha mawasiliano anachosema kilipatikana kwa mwanamume mmoja aliyenaswa na wafuasi wa vuguvugu hilo, wakimshuku kuwa miongoni mwa waliokuwa wanaendeleza uhuni dhidi yao.
Katika taarifa aliyotundika katika ukurasa wake wa Facebook, Bw Sifuna, aliye pia Seneta wa Nairobi anahadithia matukio ya Jumapili, Agosti 16, 2026 ambako msafara wao katika ziara Homa Bay ulikabiliwa na ghasia na uharibifu wa kushtua.
Kufikia sasa, Kamanda wa Polisi Kaunti hiyo Lawrence Koilem amethibitisha maafa ya watu wawili, akiwemo afisa wa polisi, na majeruhi zaidi ya 45 waliokimbizwa hispitali mbali mbali.
Bw Sifuna anaeleza kwenye taarifa kwamba msafara wao ulipofika eneo la Nyandiwa, wafuasi wake walimkamata mwanamume huyo na pindi alipohojiwa alijitambulisha kama afisa wa polisi.
“Tulitwaa simu yake na tutaendelea kuizuilia. Kinachotushangaza ni aina ya simu zinazopigwa kwa simu hiyo, baadhi ya wapigaji wakijitambulisha kama maafisa wa ngazi za juu za serikali wanaoagiza simu hiyo irejeshwe,” akasema Bw Sifuna katika taarifa.
“Tunashangaa iweje simu zinazopigwa kwa chombo hicho si kutoka kwa wanafamilia wanaomtafuta mpendwa wao bali maafisa katika kitengo cha polisi.”