Familia ya Sharon yasema iko tayari kwa maridhiano na Obado
FAMILIA ya marehemu Sharon Otieno imesema iko tayari kupatanishwa na familia ya aliyekuwa Gavana wa Migori Okoth Obado, licha ya maumivu makali waliyopitia tangu marehemu alipotekwa nyara, kubakwa na kuuawa mnamo Septemba 2018.
Obado, aliyekuwa msaidizi wake wa kibinafsi Michael Oyamo na Caspal Obiero, walipatikana na hatia ya mauaji ya Sharon mnamo Julai 23, 2026.
Katika taarifa ya athari kwa waathiriwa iliyowasilishwa mahakamani, wazazi wa Sharon walisema hawana chuki dhidi ya familia ya Obado na wanatumaini juhudi za maridhiano zitaendelea.
Familia hiyo ilieleza kuwa mkutano wa maridhiano ulifanyika Agosti ukiongozwa na kaka yake Obado, Dominic Peter Akugo, pamoja na Daudi Okoth na Lenah Awino.
Wazazi wa Sharon, Douglas Zacharia Otieno na Melinda Auma, walihudhuria pamoja na jamaa wengine wa familia.
Familia ya Sharon pia ina matumaini kuwa Obado atatimiza ahadi aliyompa Sharon kabla ya kifo chake ya kumnunulia ardhi na kumjengea nyumba.
Ripoti hiyo ilisema wawakilishi wa Obado walikubali kuwa ahadi hizo zilikuwepo na walijitolea kuhakikisha zitatimizwa kwa manufaa ya watoto watatu wa Sharon, ambao sasa wanalelewa na wazazi wake.
Watoto hao wana umri wa miaka 12, 10 na minane.
Familia ilisema kifo cha Sharon kilivunja matumaini yao kwani alikuwa nguzo ya mustakabali bora wa familia.
Pia walieleza kuwa bado ni vigumu kuwaeleza watoto kilichompata mama yao.
Sharon alikuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Rongo akisomea stashahada ya rekodi za matibabu.
Alikuwa na umri wa miaka 26 na alikuwa mjamzito wa wiki 28 alipopoteza maisha.
Mahakama ilielezwa kuwa Sharon alikuwa amepokea vitisho vya kuuawa kabla ya kifo chake, hali iliyomlazimu hata kutorokea Tanzania kwa muda kabla ya kurejea nchini.
Jaji Cecilia Githua aliamua kuwa upande wa mashtaka ulithibitisha kuwepo kwa njama iliyohusisha Obado, Oyamo na Obiero.
Mahakama ilikubaliana kuwa ujauzito wa Sharon na uhusiano wake na Obado vilitishia hadhi ya kisiasa ya gavana huyo wa zamani.
Hata hivyo, wazazi wa Sharon wanasema maridhiano hayawezi kufuta maumivu waliyonayo.
Wanaendelea kuhitaji usaidizi wa kisaikolojia na kifedha huku wakiwalea watoto aliowaacha Sharon.
Kesi hiyo itatajwa tena Septemba 16 wakati Obado na washtakiwa wenzake watahukumiwa.