Walinzi wa Nassir wadaiwa kufyatulia vijana risasi
WATU watatu walijeruhiwa baada ya walinzi wanaodaiwa kuwa wa Gavana wa Mombasa, Abdulswamad Nassir kufyatua risasi katika hafla ya umma katika Uwanja wa Bomu, Changamwe, Mombasa, Ijumaa alasiri.
Tukio hilo lilitokea wakati wa mkutano wa kuhamasisha wananchi kuhusu mpango wa Biashara Mtaani, unaoendeshwa kupitia Hazina ya Mzunguko ya Kaunti ya Mombasa kwa wakazi wa Changamwe na Jomvu.
Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Mombasa, Stella Cherono alisema uchunguzi umeanzishwa na akawataka wote wenye taarifa kutoa kwa polisi.
“Tunachunguza tukio ambapo watu watatu walipigwa risasi na kujeruhiwa katika Uwanja wa Bomu. Tunawaomba wahusika wote kutoa taarifa uchunguzi ukiendelea,” alisema Bi Cherono.
Alisema vijana hao watatu walijeruhiwa kwa risasi na kukimbizwa katika kituo cha afya kilicho karibu, huku baadhi wakihamishiwa katika Hospitali ya Coast General kwa matibabu zaidi.
Walioshuhudia walisema kundi la vijana lilimsogelea gavana likiimba “Wantam”, na walinzi wake wakaingilia kati na kufyatua risasi kadhaa.
Afisa mmoja aliyekuwa kwenye hafla hiyo alisema polisi waliokota maganda kadhaa ya risasi eneo la tukio.
Mwanaharakati wa haki za binadamu, Francis Ouma alilaani tukio hilo na kutaka uchunguzi kufanywa kuhusu matumizi ya bunduki dhidi ya raia.
Alitaka IPOA kuchunguza na kubaini waliowafyatulia risasi vijana hao.