Kindiki asema atazima kabisa nyota ya Gachagua Mlimani
NAIBU Rais Kithure Kindiki amesema yuko tayari kumkabili mtangulizi wake Rigathi Gachagua katika vita vinavyozidi kupamba moto vya kudhibiti siasa za Mlima Kenya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Prof Kindiki na Bw Gachagua wanadai kuwa wana ushawishi mkubwa katika eneo hilo lenye wapigakura wengi, huku kila mmoja akijigamba kuwa ana uwezo wa kumbwaga mwenzake katika uchaguzi ujao.
Bw Gachagua ameapa kumzuia Rais William Ruto kupata uungwaji mkono Mlima Kenya, huku Prof Kindiki akijenga mtandao wa kisiasa wa kuzuia upinzani kutwaa eneo hilo.
Jambo moja linalowaunganisha wapinzani hao ni juhudi za kuunganisha Mlima Kenya, lakini kila mmoja akitaka umoja huo umfaidi kisiasa.
Jumamosi, Prof Kindiki aliendeleza kampeni zake za kuimarisha ushawishi wake Mlima Kenya Mashariki alipokutana na zaidi ya viongozi 20,000 wa mashinani kutoka Meru, Tharaka Nithi, Embu na Isiolo katika Uwanja wa Kinoru.
Mkutano huo uliwahusisha magavana, maseneta, wabunge, wazee wa vijiji, wahamasishaji wa afya ya jamii, madiwani wa sasa na wa zamani.
Ulijiri siku moja baada ya Naibu Rais kukutana na maafisa 15,000 wa UDA wanaosimamia vituo vya kupigia kura, ambao aliwataka kuwa mabalozi wa chama hicho tawala.
Prof Kindiki alisema atafuta ushawishi wa upinzani katika kipindi cha mwaka mmoja kuelekea uchaguzi, akidai ana uzoefu mkubwa wa kampeni kuliko Bw Gachagua.
“Upinzani usithubutu kunichokoza. Gachagua amekuwa akiona mambo ni rahisi Mlima Kenya kwa sababu sisi tulikuwa tumejishughulisha na kazi huku wao wakifanya kampeni,” alisema.
Alisema amewahi kuendesha kampeni za urais katika Mlima Kenya na kushinda.
“Wakati kampeni zitaanza, kura zitamiminika kwenye kapu la Rais. Bila kujali yaliyotokea Ol Kalou, tutashinda upinzani 2027,” alisema.
Prof Kindiki pia alimkejeli kiongozi wa DCP akimtaja kama “simba wa karatasi” na kumtaka akabiliane naye moja kwa moja.
“Tuonane ana kwa ana na tushindane kama wanaume ili kutofautisha kiongozi wa kweli na bandia. Wale wanaojigamba ni simba wa karatasi,” alisema.
Naibu Rais alisema mikutano yake na viongozi wa mashinani inalenga kuunda mtandao wa wafuasi ambao wataweza kueleza mafanikio ya serikali ya Rais Ruto.
Alisema viongozi hao watakuwa mabalozi wa serikali katika maeneo yao na kuwafahamisha wananchi kuhusu utekelezaji wa Ajenda ya Mabadiliko kutoka Chini kwenda Juu.
Prof Kindiki aliorodhesha mafanikio ambayo serikali inadai imepata katika miaka minne, yakiwemo ruzuku za kilimo, kuajiriwa kwa zaidi ya walimu 100,000 na utulivu wa thamani ya shilingi dhidi ya dola.
Pia alitaja kupungua kwa bei ya unga na mabadiliko katika huduma za afya kupitia Mamlaka ya Afya ya Jamii.
Katika michezo, alisema serikali inajenga Uwanja wa Talanta na viwanja vingine 33 katika maeneo mbalimbali nchini.
Prof Kindiki pia aliwataka wakazi kuunga mkono msimamo wa mabaraza ya wazee wa Mlima Kenya Mashariki wa kutaka eneo hilo liwe na msimamo mmoja wa kisiasa kuunga serikali.
“Mlima Kenya ni mmoja kisiasa, kijamii, kiuchumi na kitamaduni. Ni watu wachache wanaotaka kutugawanya,” alisema.
Magavana Cecily Mbarire wa Embu, Muthomi Njuki wa Tharaka Nithi na Isaac Mutuma wa Meru waliahidi kushirikiana na Prof Kindiki kuunganisha eneo hilo kumuunga mkono Rais Ruto.
Gavana Mbarire alisema wakati umefika kwa wakazi wa Mlima Kenya Magharibi kuonyesha ikiwa wanaweza kuthamini uhusiano uliopo kati ya maeneo hayo.
Gavana Njuki alisema watasaidia kuimarisha uungwaji mkono wa Naibu Rais na Rais Ruto.
“Ni msimamo wetu kwamba Kindiki abaki Naibu Rais hata baada ya 2027,” alisema.