Makala

Mtoto, 4, alivyounganishwa na mamake aliyefurushwa Saudi Arabia

Na FRIDAH OKACHI August 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MTOTO mwenye umri wa miaka minne, Precious Wambui, ameunganishwa tena na mamake Kenya baada ya kuishi Saudi Arabia kwa miaka mitatu kufuatia kufurushwa kwa mamake, Penina Wanjiru, 2025.

Precious aliwasili Nairobi Jumatatu na kukutanishwa na mamake katika afisi za Idara ya Serikali ya Masuala ya Wakenya Wanaoishi Nje ya Nchi.

Bi Wanjiru alisema anafurahi kurejeshewa mwanawe baada ya kipindi kigumu cha kutengana.

“Nina furaha sana kupata mtoto wangu. Haikuwa rahisi na nimekuwa mgonjwa, lakini sasa nitakuwa sawa. Nashukuru idara za serikali zilizotusaidia,” alisema.

Katibu wa Idara ya Huduma za Watoto, Carren Ogeng’o, mama Precious, Penina Wanjiru, na Katibu wa Idara ya Masuala ya Diaspora, Roselyn Njogu, wakati wa makabidhiano ya Baby Precious katika ofisi ya Idara ya Masuala ya Diaspora, Agosti 24, 2026. Picha|Fridah Okachi

Katibu Mkuu wa Masuala ya Wanaoishi Nchi za Nje Roselyn Njogu alisema serikali ililazimika kuthibitisha uraia wa mtoto na uhusiano wake na mamake kabla ya kuanza mchakato wa kumrejesha Kenya.

Maafisa wa ubalozi wa Kenya jijini Riyadh walishirikiana na Serikali kufanya uchunguzi wa DNA, ambao ulithibitisha kuwa Precious ni mwana wa Bi Wanjiru.

Afisa wa maslahi ya watoto pia alitumwa Saudi Arabia kuchunguza hali ya mtoto huyo, aliyekuwa akiishi na malezi ya msamaria mwema.

Bi Njogu alisema idara yake imewarejesha watoto wanane nchini tangu kuanzishwa kwake 2022.

Serikali itaendelea kufuatilia familia hiyo kuhakikisha Precious anapata mazingira salama na huduma zinazohitajika.