Kimataifa

Serikali Zambia yazuia upinzani kuwasilisha kesi kupinga matokeo; yafunga mahakama kuu

Na REUTERS August 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

LUSAKA, Zambia:

SERIKALI ya Zambia ilifunga mahakama kuu za nchi hiyo Jumatatu, ili kuwazuia watu kuingia katika majengo hayo siku ya mwisho ambayo upinzani ungeweza kuwasilisha kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi wenye utata uliofanyika mwezi huu.

Barua kutoka kwa msimamizi mkuu wa idara ya mahakama, ambao Reuters iliona, ilisema kwamba, “kwa sababu za kiusalama, wafanyakazi wote wanashauriwa kutofika kazini leo.”

Msemaji wa Polisi Godfrey Chilabi aliiambia Reuters kwamba tathmini za kiusalama zilikuwa zikiendelea, lakini akakataa kutoa maelezo zaidi.

Msemaji wa idara ya mahakama hakupatikana kutoa maoni.

Kiongozi wa upinzani Brian Mundubile alisema wiki iliyopita kwamba alikuwa akipanga kuwasilisha kesi katika Mahakama ya Kikatiba kupinga matokeo ya uchaguzi wa Agosti 13, ambapo alishika nafasi ya pili nyuma ya Rais Hakainde Hichilema.

Mwisho wa kuwasilisha kesi kama hiyo ni siku saba baada ya kutangazwa kwa matokeo, muda ambao ungeisha mapema Jumanne.

Katika majengo ya Mahakama ya Juu jijini Lusaka, ambako pia kuna Mahakama ya Kikatiba, milango yote ilikuwa imefungwa huku polisi wakionekana ndani ya eneo hilo.

Hichilema alichaguliwa tena kwa asilimia 60 ya kura katika taifa hilo kusini mwa Afrika tajiri kwa shaba.

Hata hivyo, ripoti mbili za waangalizi huru zilipata dalili kwamba idadi ya kura alizopewa Hichilema huenda ziliongezwa.

Hichilema amekanusha madai yoyote ya udanganyifu ili kuwahi ushindi.

Baada ya kukamatwa kwa baadhi ya washirika wake, Mundubile aliitwa na polisi wiki iliyopita kwa mahojiano kuhusiana na madai ya vitisho kwa usalama wa taifa, madai ambayo anasema yalibuniwa.

Wachanganuzi na mawakili wa haki za binadamu walisema wanashuku kuwa huenda akazuiwa kuwasilisha kesi yake, ingawa chama cha Hichilema kimesema Mundubile yuko huru kutumia njia za kisheria zinazopatikana.

“Tunajaribu kadri tuwezavyo kuhakikisha kesi hiyo inawasilishwa, lakini tutaona jinsi mambo yatakavyokwenda,” alisema Rais wa New Heritage Party, Chishala Kateka, ambaye chama chake ipo pia katika muungano wa upinzani unaomuunga mkono Mundubile.