Kindiki aapa kutoana jasho na ODM kutetea wadhifa wake 2027
NAIBU Rais, Profesa Kithure Kindiki Ijumaa aliambia chama cha Orange Democratic Movement (ODM), kinachoongozwa na Seneta wa Siaya Oburu Oginga, kwamba hawezi kuondolewa kirahisi, na kwamba atapambana ili kuhifadhi wadhifa wake.
Kauli hiyo ilitolewa huku akimshambulia pia kiongozi wa Wiper Democratic Movement, Kalonzo Musyoka, akimtaka asahau ndoto ya urais.
“Wadhifa wa Naibu Rais hauko wazi, na ODM inapaswa kuusahau,” alisema Profesa Kindiki.
Alizungumza katika Uwanja wa Nembure, Kaunti ya Embu, alipokutana na viongozi 20,000 wa mashinani kutoka eneo hilo.
Aliambia ODM kwamba hata mwaka 2027 atakuwa mgombea mwenza wa Rais William Ruto, ambaye anatarajiwa kutetea muhula wake wa pili.
“Mimi ni mtu mgumu sana na hawawezi kuniondoa katika kiti changu,” alisema akiwarejelea viongozi wa ODM.
Katika miezi ya hivi majuzi, mjadala kuhusu wadhifa wa Naibu Rais umeongezeka huku viongozi kadhaa ndani ya serikali jumuishi wakionyesha nia ya kuumezea mate.
Miongoni mwa waliotajwa kutamani wadhifa huo ni Oburu Oginga, Mawaziri Wycliffe Oparanya na Hassan Joho, pamoja na Spika wa Bunge la Taifa Moses Wetang’ula.
Akiwa Embu, Prof Kindiki alieleza imani yake kuwa Rais Ruto atashinda uchaguzi mkuu wa mwaka 2027 na kuwaonya viongozi wa upinzani kujiandaa kwa mapambano makali ya kisiasa.
“Siwezi kuruhusu watu wetu watoke serikalini na kuingia upinzani. Baadhi ya wanaosema tutahudumu muhula mmoja hata hawatakuwa kwenye kura.
Wanataka kutuletea watu ambao hawana rekodi yoyote ya maendeleo, hawajabadilisha maeneo yao wala kujulikana kwa maendeleo. Hatutaki kubahatisha. Tunajua tunakopeleka taifa hili,” alisema.
Prof Kindiki aliwataka viongozi wa upinzani kueleza rekodi zao za maendeleo. Aliwahimiza wakazi wa Embu kutovutwa na misemo ya kisiasa bali wawapime viongozi kwa misingi ya yale waliyofanya walipokuwa madarakani.
Alisema serikali ya Kenya Kwanza imepiga hatua kubwa katika kaunti zote 47 tangu ilipoingia madarakani mwaka 2022 na iko tayari kutetea rekodi yake mbele ya wananchi.
“Kiwango cha maendeleo tulichofikia si kile tulichokuta mwaka 2022 tulipoingia madarakani. Kazi imefanyika na wananchi wanaweza kuiona,” alisema.
Naibu Rais alisema yuko tayari kukutana na wananchi wa Embu na Wakenya wote kueleza mafanikio ya serikali katika sekta za kilimo, elimu, afya, miundombinu na nyanja nyingine muhimu.
“Niko tayari kueleza kwa wananchi kile ambacho serikali imefanya kubadilisha nchi hii na kuwawezesha wananchi kiuchumi,” alisema.
Aliwataka wakosoaji wa serikali pia waeleze walichofanikisha walipokuwa katika nyadhifa za umma.
“Waambie wananchi walifanya nini walipokuwa na mamlaka makubwa zamani. Ukweli ni kwamba hawana chochote cha kuonyesha,” alisema.
Kuhusu kilimo, Kindiki alisema serikali imeboresha bei za kahawa na maziwa. Alisema wakulima wa kahawa sasa wanapata kati ya Sh120 na Sh150 kwa kilo, huku bei ya lita moja ya maziwa ikiongezeka kutoka Sh33 hadi Sh50.
Aliongeza kuwa bei ya mbolea ilishuka kutoka Sh7,000 mwaka 2022 hadi Sh3,500, baadaye Sh2,500 na sasa Sh2,000 baada ya punguzo zaidi la Sh500.