Kiti kinachojaa mikosi Afrika Mashariki
Kujiuzulu kwa Makamu wa Rais wa Tanzania, Dkt Emmanuel Nchimbi na hatimaye kufukuzwa katika chama tawala cha CCM kumefufua mjadala mkubwa kuhusu kiti cha wagombea wenza na wasaidizi wakuu wa nchi katika Afrika Mashariki.
Ingawa mazingira ya kuondoka kwake yanaonekana tofauti na yale yaliyomkumba aliyekuwa Naibu Rais wa Kenya Rigathi Gachagua, tukio hilo limeibua swali moja muhimu: Je, kiti cha makamu wa rais au naibu rais kimegeuka kuwa kiti cha mikosi na laana katika siasa za Afrika Mashariki?
Dkt Nchimbi alitangaza kuwa ataondoka rasmi madarakani Septemba 4, 2026, chini ya mwaka mmoja tangu aapishwe kushika nafasi hiyo.
Katika barua yake kwa Rais Samia Suluhu Hassan, alieleza kuwa uamuzi wake unatokana na ahadi aliyompa rais kwamba angeendelea kuhudumu kwa uaminifu na angeondoka pale ambapo rais angeona kuna haja ya kufanya mabadiliko.
Kauli hiyo haikueleza wazi kama kulikuwa na mgogoro kati yake na Rais Samia hadi siku moja baadaye alipotimuliwa chama tawala kwa kile kilichotajwa kama kukosa nidhamu. Hata hivyo, kujiuzulu kwake kumekuja baada ya miezi ya tetesi za kisiasa kuhusu nafasi yake ndani ya serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM), jambo ambalo limeongeza uzito wa kisiasa wa tukio hilo.
Kwa Kenya, kuondoka kwa Nchimbi kunakumbusha mzozo mkubwa uliotikisa utawala wa Rais William Ruto na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua. Tofauti kubwa ni kwamba Gachagua hakujiondoa mwenyewe bali aliondolewa madarakani kupitia mchakato wa bunge na Seneti.
Kisa cha Kenya kilionyesha jinsi tofauti za kisiasa kati ya rais na msaidizi wake zinaweza kubadilika kutoka migogoro ya ndani hadi kuwa mgogoro wa kikatiba unaogusa utulivu wa taifa.
Kwa Tanzania pia, iliibuka kuwa kuondoka kwa Nchimbi kulisababishwa na mzozo wa aina hiyo. Kuna tetesi kwamba alilazimika kujiuzulu alipobaini kuwa chama kilinuia kumtimua kwa kile kinachotajwa kama kukaidi mwelekeo wa utawala.
Kwa miaka mingi, siasa za Sudan Kusini zimezunguka mikataba ya kugawana madaraka, miungano ya kisiasa na migogoro ya mamlaka kati ya viongozi wakuu wa serikali.
Tajiriba ya Sudan Kusini inaonyesha kuwa nafasi za wasaidizi wa rais si suala la watu binafsi pekee, bali ni sehemu muhimu ya uthabiti wa kisiasa wa nchi.
Mahusiano yanapobadilika ndani ya uongozi wa juu, athari zake huweza kugusa usalama wa taifa na mustakabali wa serikali.
Matukio ya Tanzania, Kenya na Sudan Kusini yanaweza kuwa tofauti kwa sura, lakini yanaonyesha changamoto moja ya msingi.
Mara nyingi manaibu rais huingia madarakani wakiwa washirika wakuu wa rais, lakini baada ya muda, tofauti za kisiasa, matarajio ya urithi wa madaraka au ushindani wa ushawishi ndani ya vyama tawala huibuka.
Matokeo yake yanaweza kuwa kujiuzulu, kuondolewa madarakani au kukaziwa ushawishi wao katika serikali. Hali hii imefanya kiti cha makamu wa rais au naibu rais kuonekana kama mojawapo ya nyadhifa hatari zaidi kwa maisha ya kisiasa.
Mjadala huu unajiri huku Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ikiendelea kusukuma mbele mpango wa Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki kupitia hatua ya Shirikisho la Muungano.Iwapo ni laana au la, ni wazi kuwa kiti cha makamu wa rais na naibu rais kimekuwa na changamoto nyingi kisiasa.