Makala

Hofu Ziwa Bogoria likikaribia kuungana na Ziwa Baringo

Na FLORAH KOECH August 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KUNA uwezekano wa Ziwa Bogoria na Ziwa Baringo kuungana hivi karibuni huku umbali kati yao ukipungua hadi chini ya kilomita tatu kutoka kilomita 20.

Hali hiyo imezua hofu ya janga la kimazingira kwa kuwa maziwa hayo mawili yana sifa tofauti. Ziwa Baringo lina maji yasiyo na chumvi, huku Bogoria likiwa na maji yenye chumvi.

Kwa zaidi ya muongo mmoja, wakazi wa Loboi, Baringo Kusini, wamekuwa wakishuhudia Ziwa Bogoria likipanuka na kuelekea kwenye makazi, mashamba na biashara zao.

Maji hayo tayari yamemeza nyumba, kituo cha afya, maeneo ya malisho na maelfu ya ekari za mashamba.

Wataalamu wanaonya kuwa iwapo maziwa hayo yataungana, mfumo wa ikolojia wa Baringo unaweza kuathirika pakubwa.

Samaki, viboko, mamba na jamii zinazotegemea maji ya Baringo zinaweza kuwa miongoni mwa waathiriwa.

Serikali sasa inapanga kujenga bwawa na mitaro ya kuzuia maji ya Bogoria kuelekea Baringo.

Mpango huo unajumuisha ujenzi wa tuta la kilomita tano huko Sandai, bwawa katika Mto Waseges na mtaro wa takriban kilomita 40.

Mtaro huo utatumika kuondoa maji mengi kutoka Baringo kuelekea Chemolingot na hatimaye Bonde la Suguta.

Timu ya mashirika mbalimbali, ikiwemo Idara ya Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi, Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF), Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ) na Shirika la Msalaba Mwekundu Kenya, imekuwa ikichunguza eneo hilo.

Gavana wa Baringo, Benjamin Cheboi, alisema mafuriko hayo yamezidi uwezo wa serikali ya Kaunti.

“Mafuriko haya ni makubwa sana na kama serikali ya kaunti hatuwezi kuyakabili peke yetu. Ndiyo maana tumeomba usaidizi kutoka kwa serikali ya kitaifa na washirika wengine,” alisema.

Wakazi wanasema Bogoria ilianza kupanuka kwa kasi mwaka 2010, hali iliyoongezeka mwaka 2013.

Bw Bismark Kibet alisema zaidi ya vijiji sita, kikiwemo Chepng’erechi na Kaprong’uno, vimeathirika huku Bw Jonathan Tireito akisema wakazi walidhani maji yangepungua baada ya muda.

“Tulidhani yangepungua lakini hayajapungua. Yamefunika nyumba, maeneo ya malisho, mashamba na hata zahanati yetu,” alisema Bw Tireito.

Msimamizi Mkuu wa Hifadhi ya Bogoria James Kimaru, alisema eneo la ziwa limeongezeka kutoka takriban kilomita 34 za mraba mwaka 2013 hadi karibu kilomita 45 kwa sasa.

Barabara na miundombinu mingine katika hifadhi hiyo imehamishwa, huku chemchemi za maji moto na maeneo yaliyokuwa yakivutia watalii kutazama flamingo yakizama.

Profesa Simon Onywere, mtaalamu wa mipango ya mazingira na jiolojia, alisema umbali kati ya maziwa hayo ulipungua kutoka zaidi ya kilomita 20 hapo awali hadi kilomita saba mwaka 2020 na sasa ni chini ya kilomita tatu.

“Kuungana kwa maziwa haya kumekaribia na ni suala la muda tu,” alisema.

Alisema maji mengi kutoka Mto Waseges yanaendelea kuingia Bogoria, hivyo kuongeza uwezekano wa maji yenye chumvi kuelekea Baringo.

“Ikiendelea hivi, Ziwa Baringo linaweza kuwa na maji ya chumvi na kuhatarisha samaki, viboko, mamba na jamii zinazolitegemea,” alisema.

Serikali pia inapanga kutumia maji hayo kwa unyunyizaji, huku mpango mpana ukilenga angalau ekari 100,000 katika Baringo na Turkana.

Wakati huo huo, Ziwa Baringo lenyewe limepanuka kutoka kilomita 178 za mraba hadi zaidi ya 260.

Afisa Mkuu wa Hifadhi, Bw Jackson Komen, alisema nyumba, shule, biashara na hoteli zimeathirika.