Vigogo wa ‘Broadbased’ waahidi Ruto kura milioni 7 Nyanza, Magharibi uchaguzi mkuu
WANASIASA wanaounga mkono serikali kutoka Nyanza na Magharibi wametangaza mipango ya kuendesha kampeni za pamoja kwa lengo la kumwezesha Rais William Ruto kupata kura milioni 7 maeneo hayo 2027.
Mpango huo unalenga kuvutia kura katika ngome za kisiasa za marehemu Waziri Mkuu Raila Odinga chini ya Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi.
Sehemu ya mikakati hiyo pia ni kushinikiza watengewe nafasi ya Naibu Rais.
ODM imependekeza Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya kama mmoja wa wanaoweza kuchukua nafasi ya Profesa Kithure Kindiki.
Luo Nyanza, inayojumuisha kaunti za Kisumu, Migori, Siaya na Homa Bay, ina wapiga kura milioni 2.41 kwa mujibu wa sajili ya sasa ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC).
IEBC inakadiria idadi hiyo kufikia milioni 2.78 katika uchaguzi wa Agosti 10, 2027.
Magharibi nayo ina kaunti za Kakamega, Busia, Bungoma, Vihiga na Trans Nzoia zina wapiga kura milioni 2.9 kwa sasa, huku idadi hiyo ikitarajiwa kufikia milioni 3.4 ifikapo uchaguzi ujao.
Hata hivyo, mpango huo unakabiliwa na upinzani kutoka kwa vuguvugu la Linda Mwananchi, ambalo limekuwa likipata umaarufu katika maeneo hayo.
Baadhi ya viongozi wa Magharibi, akiwemo Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi na Seneta wa Kakamega Boni Khakwale, wamejipanga kumuunga mkono Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kwa urais.
Nyanza pia inapitia mabadiliko makubwa ya kisiasa tangu kifo cha Bw Odinga. Gavana wa Siaya James Orengo na Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi wameungana na Bw Sifuna kupinga ushawishi wa uongozi wa sasa wa ODM.
Hata hivyo, washirika wa Rais Ruto wanasema wataunganisha jamii za Luo na Luhya ili kumuunga mkono katika uchaguzi wa 2027.
Jamii hizo kwa kiasi kikubwa zilimuunga mkono Bw Odinga katika uchaguzi wa 2022.