IEBC inavyojiandaa kwa uchaguzi wa 2027
TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imeingia katika awamu muhimu ya maandalizi ya uchaguzi mkuu wa 2027 huku ikiwa na chini ya mwaka mmoja kuhakikisha changamoto zilizopo zinatatuliwa.
Mwenyekiti wa IEBC, Erastus Ethekon, amesema tume hiyo inaendelea na maandalizi mbalimbali, ikiwemo usajili wa wapigakura, teknolojia, ununuzi wa vifaa, elimu ya wapigakura, usafirishaji, kuajiri na kuwapa mafunzo maafisa wa uchaguzi.
Bw Ethekon alisema tume hiyo tayari imeanza michakato mikuu ya ununuzi wa teknolojia, karatasi za kura na vifaa vingine vitakavyohitajika katika uchaguzi.
Alisema awamu ya kwanza ya Usajili Endelevu wa Wapigakura ilisajili wapigakura wapya milioni 2.3 dhidi ya lengo la milioni 2.5.
Kufikia Agosti 17, 2026, jumla ya wapigakura wapya 2,920,600 walikuwa wamesajiliwa, huku IEBC ikilenga kuwa na orodha ya wapigakura takriban milioni 28.5 mwaka 2027.
Hata hivyo, tume hiyo inakabiliwa na changamoto kadhaa, zikiwemo ukosefu wa fedha, ucheleweshaji wa sheria muhimu na wasiwasi kuhusu vurugu za kisiasa.
Katika mahojiano na Taifa Jumapili, Bw Ethekon alisema tume hiyo inahitaji hadi Sh35 bilioni kukamilisha maandalizi yake.
Kuhusu madai ya upendeleo katika zabuni ya teknolojia, mwenyekiti huyo alisema hakuna kampuni ambayo imeshinda zabuni hiyo.
Alisema mchakato wa ununuzi unaendelea kwa kuzingatia Katiba na sheria za ununuzi wa umma.
“Kufikia sasa, hakuna zabuni iliyotolewa kwa kampuni yoyote,” alisema.
Alisema maamuzi ya mwisho yatafanywa baada ya mchakato wa wazi na wa uwazi kukamilika.
Kuhusu madai ya upinzani kwamba IEBC inaegemea upande wa serikali, Bw Ethekon alisema tume hiyo haiwezi kuendeshwa kwa matakwa ya wanasiasa.
“Wajibu wetu si kufurahisha serikali, upinzani, vyama vya kisiasa au mtu yeyote. Wajibu wetu ni kwa Katiba na watu wa Kenya,” alisema.
Kuhusu gharama ya uchaguzi, Bw Ethekon alisema Kenya ina mfumo wa kipekee kwa sababu chaguzi sita hufanyika siku moja; wa Rais, Bunge la Kitaifa, Seneti, ugavana, Mwakilishi wa Wadi na mwakilishi wa wanawake.
Alisema gharama hizo pia zinahusisha usafirishaji, teknolojia, karatasi za kura, maafisa wa uchaguzi, elimu ya wapigakura, usalama na vifaa.
“Tunaomba rasilimali zinazohitajika kuendesha uchaguzi unaotakiwa na Katiba,” alisema.
Kuhusu kuchelewa kwa maandalizi, mwenyekiti huyo alisema IEBC haijafikia hatua ya hofu, lakini muda sasa unapaswa kuchukuliwa kama rasilimali muhimu ya kitaifa.
“Je, tuna wasiwasi? Tuko macho. Je, tunaingiwa na hofu? Hapana,” alisema.
Alisema kuchelewesha maamuzi muhimu kunaweza kuathiri majaribio ya teknolojia, usambazaji wa vifaa, mafunzo na maandalizi ya dharura.
Bw Ethekon pia alikiri kuwa vijana wamepoteza imani kwa taasisi za uchaguzi, akisema IEBC lazima itumie njia mpya kuwafikia.
Alisema vijana wanahitaji taarifa za wazi na fursa za kuwasiliana na tume hiyo mara kwa mara, si wakati wa uchaguzi pekee.
“Imani hujengwa kupitia matendo,” alisema