Tanzania yaomboleza kifo cha mume wa Rais Samia, Hafidh Ameir Hassan
DAR ES SALAAM, Tanzania
TANZANIA inaendelea kuomboleza mauti ya Mume wa Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Hafidh Ameir Hassan.
Hassan alifariki Jumatatu asubuhi alipokuwa akipokea matibabu baada ya kuugua maradhi ya moyo.
Tangazo la kifo chake lilitolewa na Makamu wa Rais wa Tanzania Deogratius Ndejembi, aliyesema Hassan alifariki mwendo wa saa mbili asubuhi katika hospitali moja Zanzibar.
“Wananchi wenzangu, ni kwa masikitiko makubwa ninawafahamisha kuhusu kifo cha Hafidh Ameir Hassan, mume wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan,” akasema Ndejembi.
“Alifariki Septemba 7, 2026, mwendo wa saa mbili asubuhi katika Hospitali ya Emilio Mzena Memorial, Zanzibar, alipokuwa akipokea matibabu ya ugonjwa wa moyo,” akaongeza.
Makamu wa Rais alitoa pole kwa Rais Samia, familia, ndugu na marafiki wa marehemu pamoja na Watanzania wote, akisema maandalizi ya mazishi yalikuwa yashaanza katika eneo la Kizimkazi, Zanzibar.
Hafidh Ameir na Samia Suluhu walifunga ndoa 1978 na walijaliwa watoto wanne, akiwemo Wanu Hafidh Ameir, ambaye ni mwanasiasa na mbunge Tanzania.
Hassan alikuwa msomi na mtaalamu wa kilimo, lakini alijulikana zaidi kwa kutopenda kujihusisha na shughuli za hadhara au za umma.
Katika kipindi chake kama Mume wa Rais, aliishi maisha ya faragha na hakujihusisha sana na mitandao ya kijamii, kiasi kwamba umma ulijua machache kumhusu.
Baada ya kifo chake, viongozi mbalimbali, akiwemo Rais wa Kenya William Ruto, walituma rambirambi kwa Rais Samia.
Rais Ruto alimsifu Hassan kuwa baba mpendwa na mwana mashuhuri wa Tanzania, akitoa pole kwa niaba yake binafsi na Wakenya wote.
“Nimepokea kwa masikitiko makubwa habari za kifo cha Hafidh Ameir Hassan, mume wa Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” akasema Rais Ruto.
“Kenya iko pamoja na ndugu na dada zetu wa Tanzania katika kipindi hiki cha maombolezo. Mwenyezi Mungu amfariji Rais Samia na familia yake, awape nguvu katika kipindi hiki kigumu na ailaze roho ya Hafidh Ameir Hassan mahali pema peponi,” akaongeza Rais Ruto.
Bado viongozi wengine kutoka ndani na nje ya Tanzania walikuwa wakiendelea kutuma rambirambi kwa familia ya Rais Samia.