Mahangaiko tele raia wa kigeni wakihofia kuendelea kukaa nchini
HOFU, sintofahamu na wasiwasi zimetanda miongoni mwa raia wa kigeni wanaofanya biashara ndogo ndogo nchini kufuatia agizo la serikali linalowataka warekebishe hati zao za uhamiaji na vibali vya kufanya kazi ndani ya siku 90.
Kwa Archade Nshimirimana, raia wa Burundi mwenye umri wa miaka 34 anayeishi Kitengela, maisha aliyojenga kwa zaidi ya miaka 11 yanaonekana kutikiswa na mwelekeo mpya wa serikali. Nshimirimana aliwasili Kenya kama mkimbizi mwaka 2015 akitoroka ghasia za kisiasa nchini Burundi.
Alianza maisha kama kinyozi kabla ya kusomea huduma za urembo na hatimaye kufungua saluni yake.
“Nimejenga maisha yangu hapa. Nimeoa Mkenya na nimekuwa nikisaidia wazazi wangu walioko Burundi. Wiki iliyopita imejaa hofu na mkanganyiko,” alisema.
Kitengela, ambayo imekuwa makazi ya maelfu ya wageni kutoka Burundi, Congo, Rwanda na Uganda, ilishuhudia biashara nyingi zinazomilikiwa na wageni zikifungwa kwa muda baada ya tangazo hilo. Wageni wengi hushughulika na biashara za vyakula, saluni, ushonaji na huduma za bodaboda.
Hali kama hiyo imeshuhudiwa Nakuru ambako wafanyabiashara wengi wa kigeni wanakiri kuwa wameathiriwa kiuchumi.
Iradukunda Samson, mwenye umri wa miaka 21 kutoka Burundi, amekuwa akiuza vibanzi mitaani kwa miaka mitatu. Mapato yake humwezesha kulipa kodi ya nyumba, kujikimu na kusaidia familia yake nyumbani.
Alisema hofu ya kushambuliwa imewafanya baadhi ya wageni kuacha kazi huku wengine wakirejea nchini mwao.
“Tuko tayari kupata vibali vinavyohitajika, lakini tunaogopa kutoka nje kwenda kufanya biashara,” alisema.
Katika mtaa wa Bondeni, Nakuru, Uragiwenimama Jeondodieu anayefahamika kama John, huendesha kibanda pamoja na mke wake Mkenya.
Alisema wageni wengi wameishi kwa amani na wenyeji kwa miaka mingi na wanapaswa kupewa nafasi ya kurekebisha stakabadhi zao badala ya kuonekana kama wahalifu.
Wakati huo huo, serikali ya Burundi imeitaka Kenya kuhakikisha usalama wa raia wak na maafisa wa serikali ya Kenya wamewahakikishia wageni usalama wao huku wakiwataka kutumia muda wa siku 90 kutafuta vibali na hati zinazohitajika.
Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi alifafanua kuwa muda huo haukusudiwi kuwafukuza wageni bali kuwapa nafasi ya kutii sheria.
Licha ya hakikisho hilo, wengi bado wanaishi kwa taharuki, wakisubiri kuona kitakachotokea baada ya muda wa siku 90 kukamilika.
Baadhi yao wana matumaini kuwa wataendelea kuishi na kufanya kazi Kenya, nchi ambayo wameiita nyumbani kwa miaka mingi.